Je wajua nyumba ijengwe vipi ihimili mabadiliko ya Tabianchi?
Je wajua nyumba ijengwe vipi ihimili mabadiliko ya Tabianchi?
Muongo uliopita ulitajwa kuwa wenye viwango vya juu vya joto zaidi katika historia. Majanga yakiwemo moto wa nyika, mafuriko na vimbunga vinazidi kuongezeka huku viwango vya gesi chafuzi vikiwa ni asilimia 62 zaidi tangu wakati mazungumzo kuhusu mabadiliko ya tabianchi yalipoanza mwaka 1990.
Ushahidi uko wazi kuwa tuko mbioni kuishi kuambatana na mabadliko ya tabianchi.
Ripoti mpya ya shirika la mazingira la Umoja wa Mataifa, UNEP inaonesha jinsi nyumba zinaweza kujengwa hasa kwenye nchini zinazoendelea
Hebu tumulike njia tano za ujenzi wa majengo yanayoweza kuhimili mabadiliko ya tabianchi kama ilivyochapishwa katika wavuti wa UNEP.
Kujenga kwa kuzingatia viwango vya joto
Utafiti unaonesha kuwa ifikapo mwaka 2050 watu bilioni 1.6 wanaoishi ndani ya zaidi miji 970, mara kwa mara watakumbwa na viwango vya juu vya joto hali ambayo itayaweka maisha ya wakazi wa miji hii katka hatari kubwa.
Lakini mazingira yana suluhu zake. Jamii zinaweza kubuni misitu ya mijini na maeneo yenye miti kupungzua joto mijini kwa kuwa miti huleta kivuli na hali ya ubaridi.
Miundo ya mijengo pia nayo inaweza kuchangia kupunguza joto ndani ya majengo. Kwa mfano nyumba zinazojengwa kwa saruji nzito na kwa vifaa vingine vizito hutumiwa China, Chile na Misri kupunguza joto.
Kujenga kwa kuzingatia ukame
Mabadiliko ya tabianchi yameathiri misimu ya mvua kote duniani
Uhifadhi ya maji ya mvua na mifumo inayotumiwa kuyakusanya maji ni njia kuu za kuhifadhi maji wakati wa ukame na kupunguza hatari ya kutokea mafuriko wakati misimu ya mvua nyingi.
Maji yaliyokusanywa yanaweza kuhifadhiwa kwenye matanki na kutumiwa nyumbani wakati wa ukame.
Njia nyingine rahisi ya kukabalina na ukame na mafuriko ni kwa kupanda miti au mimea mingine nje ya majengo. Mizizi ya miti hii husadia maji kufyonzwa kwenye udongo na hivyo hupunguza hatari ya kutokea mafurko.
Kujenga kwa kuzingatia mafuriko sehemu za pwani na kupanda viwango maji ya bahari
Mwaka 2025 watu milioni 410 walio maeneo ya pwani watakuwa katika hatari ya mafuriko na kuongeza viwango vya maji ya bahari.
Huko Kerala, India nyumba zinazoweza kustahimili mafuriko zinajengwa juu ya nguzo ili kuruhusu maji ya mafuriko kupita chini yake.
Kwenye pwani ya Malaysia nyumba zimeinuliwa mita mbili juu kuruhusu maji kupita na miti kumea chini yake.
Mbinu moja iliyopendekezwa Bangladesh ni kujengwa nyumba ambayo itakalia nguzo zenye matanki yanayoweza kuelea wakati wa mafuriko.
Jengo hilo linaweza kutumiwa kama kituo cha kijamii na kama makazi ya dharura wakati wa mafuriko.
Kujenga kwa kuzingatia vimbunga na upepo mkali
Vimbunga na mawimbi vinatarajiwa kutokea mara kwa mara kufuatia mabadiliko ya tabianchi.
Vinaweza kuathiri majengo kwa njia nyingi kama vile kwa kung’oa mapaa na hata kuharibu misingi ya majengo.
Miundo ya mapaa huwa na umuhimu mkubwa. Uthabiti kutoka msingi wa nyumba hadi kwenye paa ni kati ya njia za kuhakikisha mapaa yanastahimili upepo.
Kujenga kwa kuzingatia baridi
Hii inahusu kujengwa kwa namna ambayo nyumba inaweza kupata joto na kuhifadhi joto la ndani.
Mapaa, kuta na madirisha vinaweza kujengwa kwa namna ambayo vitazuia kupotea kwa joto .
Majengo pia yanaweza kujengwa wa kwa njia ambayo yatakuwa rahisi kumulikwa na jua pia kuta zinastahili kupakwa rangi nyeusi.
Mapaa yanayoweza kusaidia mimea kumea juu yake hutumiwa kwenye miji mingi kote duniani na huonekana kuwa suluhu kwa kuleta ubaridi msimu wa joto na joto wakati wa msimu wa baridi.