Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hakuna faida ya kungonoka mapema- Kijana balehe

Shirika la afya duniani WHO linawachagiza vijana barubaru kufanya mazoezi ya viungo na zaidi kwa ajili ya afya na mustakabali wao
Unsplash/Paul Proshin
Shirika la afya duniani WHO linawachagiza vijana barubaru kufanya mazoezi ya viungo na zaidi kwa ajili ya afya na mustakabali wao

Hakuna faida ya kungonoka mapema- Kijana balehe

Utamaduni na Elimu

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto -UNICEF nchini Uganda linafadhili mradi wa Mama kwa Mama ambao unajengea uwezo maafisa wa ustawi wa jamii wanaopita kila kaya maskini kusaka  barubaru na vijana balehe waliopata mimba katika umri mdogo na kuwapatia stadi za ufundi ili  hatimaye waweze kujipatia kipato na kubadilisha maisha yao


Wilayani Kasese nchini Uganda, video ya shirika la UNICEF imeanza kwa kuonesha binti mwenye umri wa miaka 14 kwa jina la Mary akiwa amembeba mwanae mgongoni na kuni mkononi akiingia ndani ya nyumba yao. Kisha akipuliza moto kupika huku mwanae akiwa gongoni. 
 
Mary (sio jina lake halisi), yeye alipata mimba akiwa kidato cha kwanza kitendo kilicho wahuzunisha sana wazazi wake kwani aliacha shule na kukaa nyumbani. 
 
Maisha yake yaliokolewa na mfanyakazi wa ustawi wa jamii aliyepatiwa mafunzo na UNICEF kupitia mradi wa Mama kwa Mama ili kusaida wasichana wenye madhila kama Mary. Stadi ni pamoja kufuma vikapu, kuoka keki ili wapate fedha za kujikimu. Na ndoto ya kurejea shuleni imerejea… 
  
"Nataka kurudi shule, sababu nataka kuja kuwa muuguzi ili niwatibu wasichana wengine. Mtoto wangu akiwa mkubwa nataka kurudi shule."  
 
Na  anatuma ujumbe kwa barubaru wengine "Hakuna uzuri wowote wakushiriki ngono katika umri mdogo kama wetu sababu utapata mimba na ndoto zako zote zitasimama, wenzako watakuwa wanaendelea na shule wakati wewe umekaa nyumbani ukilea mtoto” 
 
Wilaya ya Kasese ina  jumla ya vikundi 47 ambavyo vinatoa ufundi stadi ili kuwapa uwezo mabinti hawa wa kuwa na mwanzo mpya.  
 
Mary nuru imemwangazia tena anafunua madaftari yake ajisomeee maana amepata anarejea shuleni kuendelea na masomo ili aweze kutimiza ndoto yake ya kuwa muuguzi.