Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Taka ngumu ikiwemo plastiki ni mtihani mkubwa Cox's Bazar, IOM yachukua hatua

Kijana wa miaka 12 nchini Bangladesh akichambua taka za plastiki bila kuwa na kinga yoyote, na hiyo ni kazi yake inayomuwezesha kusaidia familia yake
© UNICEF/Parvez Ahmad
Kijana wa miaka 12 nchini Bangladesh akichambua taka za plastiki bila kuwa na kinga yoyote, na hiyo ni kazi yake inayomuwezesha kusaidia familia yake

Taka ngumu ikiwemo plastiki ni mtihani mkubwa Cox's Bazar, IOM yachukua hatua

Tabianchi na mazingira

Udhibiti wa taka ngumu ikiwemo za plastiki ni changamoto kubwa katika kambi ya wakimbizi wa Rohingya ya Cox’s Bazar nchini Bangladesh, na hasa kwa kuzingatia kwamba kambi hiyo ina msongamano na hakuna shemu maalum ya kutupa limesema shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM ambalo  sasa limepata dawa mujarabu. Je ni ipi hiyo? Ungana na Flora Nducha 

Katika kambi ya wakimbizi ya Cox's Bazar IOM inasema uhaba wa maeneo ya kujenga madampo ndio chanzo kikuu cha kuzagaa kwa taka ngumu zinazozalishwa na wakimbizi hao zikiwemo za plastiki. Kwa kutambua tatizo hilo Baudoin Luce afisa ufundi wa programu ya huduma za maji safi na usafi WASH kutoka shirika la IOM anasema imebidi wachukue hatua “Kutokana na kutokuwa na maeneo program ya IOM ya WASSH Cox’s Bazar ina mkakati wa kuzitumia tena, kupunguza na kurejeleza taka hizo, ili kudhibiti  kiwango cha taka zinazotupwa majalalani. “ 

Mshirika wa IOM kampuni  DSK ndio inayoendesha program hiyo na inakusanya karibu kilo 25 za plastiki kila siku.  

Lakini mchakato mzima unafanyika vipi? Baudoin anaeleza “Hatua ya kwanza ni kukusafisha na kukausha taka hizo za plastiki, kisha tunaziweka katika machine ya kuzisaga katika vipande vidogovidogo. Na baada ya hapo tunazipeleka kwenye machine ya pili ambayo ni ya kubadili mauambile ya plastiki hizo na kuzifanya kuwa kama tambi nyembamba, na kisha tunazikatakata tena kupata chembechembe ndogondogo zaidi ambazo hatimaye zitawekwa kwenye machine maalum za kuunda bidhaa zingine za mwisho tulizokusudia.” 

Na sasa IOM ambayo imekuwa imekuwa ikitengeneza bidhaa kama alfabeti kwa ajili ya kufundishia wanafunzi kwenye kituo cha kambini hapo inafikiria kuunda bidhaa zingine zaidi kama vile vibao vyeusi vya kuandikia na  kuanzisha mradi huo katika maeneo mengine. 

Na ili kuhakikisha mradi huu haua athari kwa binadamu na mazingira IOM imeanza kufanya tathimini kwani mbali ya kudhibiti taka  inasema ni fursa nzuri ya biashara kwa wakimbizi na jamii zinazowahifadhi