Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kenya: Msaada wa pesa wa WFP waleta nuru kwa familia duni Mombasa na Nairobi 

Wakazi wa makazi ya Moroto Simitini mjini Mombasa wameathiriwa sana na athari za kiuchumi za COVID-19.
Picha: WFP/Martin Karimi
Wakazi wa makazi ya Moroto Simitini mjini Mombasa wameathiriwa sana na athari za kiuchumi za COVID-19.

Kenya: Msaada wa pesa wa WFP waleta nuru kwa familia duni Mombasa na Nairobi 

Msaada wa Kibinadamu

Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP na washirika wake wamefikiaa na msaada familia 95,000 katika makazi yasiyo rasmi mijini Nairobi na Mombasa.

Vichochoro vyembamba kwenye mteremko ulio kati ya mabanda yaliyobanana na kusongamana karibu karibu. Vichochoro hivi vina mamia ya nyumba ambazo zinaunda makazi ya Moroto Simitini. 

Kijiji hicho kiko katika mji maarufu wa pwani ya Kenya wa Mombasa, ambako shirika la WFP linatoa pesa za dharura kwa familia zilizopoteza mapato kutokana na janga la corona au COVID-19. Kila familia hupokea shilingi 4,000 za Kenya sawa na dola za Kimarekani 37 kila mwezi, kwa muda wa miezi mitatu. 

Hapa, walio karibu zaidi na ukingo wa bahari ndio maskini zaidi. Wanaishi katika mazungira duni nyumba zao zikipitiwa na mifereji ya maji.  

Taka husukumwa na maji hadi karibu na milango yao au hata pia zinapitia milangoni ikiwa hazitodhibitiwa wakati wa mafuriko. 

Mfanyikazi wa WFP, kulia, anazungumza na mkazi wa Muroto Simitini.
Picha: WFP/Martin Karimi
Mfanyikazi wa WFP, kulia, anazungumza na mkazi wa Muroto Simitini.

 

Kijiji hiki kinahifadhi takriban watu 30,000 ambao karibu wote wanafanya kazi zhali ya chini.  

Wanawake huosha na kusafisha nyumba katika maeneo jirani ili kulisha watoto wao na wanaume husafirisha bidhaa kwa mikokoteni au wakitembeza migongoni ili wapate kipato. 

Benedetta ni mama mzazi wa watoto watano ambaye hupata riziki kwa kuosha na kusafisha nyumba za majirani walio na hali nzuri.  

Tangu kuzuka kwa janga la COVID-19 amehangaika kupata ajira, kwa kuwa walinzi kwenye maeneo ya makazi  ya mjini yanayolindwa hawaruhusu mtu yeyote kutoka vijijini kuingia. 

Sasa, na ujio wa chanjo, wahudumu wa afya, walimu na wafanyikazi wa usalama wako katika msitari wa mbele kuchanjwa, wakifuatiwa na wazee na wale walio na matatizo makubwa ya kiafya.  

Hata hivyo, Benedetta mwenye umri wa miaka 35 na wenzake, watalazimika kusubiri kwa muda mrefu. 

“Siku nyingi, nilishindwa kupata kazi yoyote na nilikuwa nikirudi na kukaa kandfoni mwa Kijiji chetu, nikingojea na kutarajia kupata mtu atakayenikopesha pesa ya kununua unga”, jirani yake, Dorcas Adaye, anakumbuka maisha baada ya amri ya kusalia majumbani kuanzishwa. 

Chirindo Mwambui katika nyumba yake ambayo bado ujenzi unaendelea kwenye makazi ya Moroto Simitini.
Picha: WFP/Martin Karimi
Chirindo Mwambui katika nyumba yake ambayo bado ujenzi unaendelea kwenye makazi ya Moroto Simitini.

"Ningekaa huko hadi jioni kwa sababu sikutaka kurudi nyumbani mikono mitupu na kulazimika kujieleza kwa watoto wangu wenye njaa." 

Chirindo Mwambui anaishi na watoto wake wanne nyumba chache tu kutoka kwenye eneo la mteremko. 

Alifanya kazi kwenye mgahawa akiandalia watoto wa shule za upili chakula cha mchana.  

Kwa bahati mbaya, mgahawa ulifungwa wakati shule zililazimishwa kufungwa. Na Chirindo akapoteza kazi. 

"Ninatafuta kazi kila siku lakini sina bahati, inanibidi kukopa pesa kulisha watoto wangu," anasema. "Ikiwa siwezi kupata pesa taslimu au kununua chakula kwa mkopo, hatuna chaguo bali kunywa chai ya rangi na kulala." 

Wakazi waliokusanyika katika mitaa ya makazi yasiyo rasmi ya Mukuru Kwa Reuben mjini Nairobi.
Picha: WFP / Alessandro Abbonizio
Wakazi waliokusanyika katika mitaa ya makazi yasiyo rasmi ya Mukuru Kwa Reuben mjini Nairobi.

Katika nyumba yake kuna mashimo na nyufa na paa halijakamilika. Chumba anachoishi ni kidogo sana kina kipimo cha karibu mita 4 kwa 3.  

Kuna kitanda kimoja tu ambacho kinachukua sehemu kubwa ya chumba chenyewe, sehemu inayobaki ni jikoni na stoo ya kuhifadhi vitu.  

Ni vigumu kuzunguka au hata kupita ndani ya chumba chake kutokana na ufinyu wa shehemu yenyewe ambayo kwa sasa watu watano wanaishi hapo; Chirindo, mwanawe wa miaka 22, binti zake vijana wawili na mtoto wake wa mwisho wa kiume. 

Wanaishi katika umasikini mkubwa. 

Mwanaume akivuka majitaka na takataka katika barabara kwenye eneo la makazi yasiyo rasmi ya Mukuru Kwa Reuben mjini Nairobi.
Picha: WFP / Alessandro Abbonizio
Mwanaume akivuka majitaka na takataka katika barabara kwenye eneo la makazi yasiyo rasmi ya Mukuru Kwa Reuben mjini Nairobi.

 "Nilinunua chakula na kulipa deni yangu kutumia pesa nilizopokea kutoka WFP," anasema. “Pia nililipa karo ya shule na nilinunua nguzo na mabati ya kuezeka nyumba hii. Ingawa pesa ziliisha, ni bora kuliko makao yangu ya zamani ambayo yalitengenezwa kwa maboksi na vyandarua kwani mvua ikinyesha, kila kitu hapa kinalowana chapachapa.” 

 

Mwanamke anapitia njia nyembamba za makazi yasiyokuwa rasmi ya Huruma mjini Nairobi.
Picha: WFP / Alessandro Abbonizio
Mwanamke anapitia njia nyembamba za makazi yasiyokuwa rasmi ya Huruma mjini Nairobi.

 

"Ningependa kufungua kibanda cha chakula, ni biashara salama zaidi kwa sababu watu lazima wale," anasema. "Sitashindwa kupata pesa na nitaweza kuwatunza watoto wangu." Halafu, anauliza: "Je! Unaweza kutusaidia kuanzisha biashara ndogo ndogo ili tuweze kupata kipato kupitia jasho letu?" 

Nyakati ngumu 

Kwa kushirikiana na serikali za kaunti na kitaifa, WFP imezisaidia familia 23,000 katika makazi yasiyo rasmi ya Mombasa nusu ya mahitaji yao ya chakula ya kila mwezi kwa muda wa miezi mitatu. 

Mahitaji yao, hata hivyo, ni makubwa zaidi ya chakula tu, na changamoto za uchumi zilizosababishwa na janga la COVID-19 zinaendelea. 

Duka la vyakula lililoanzishwa katika kijiji cha Kibagare, Nairobi, kutokana na msaada wa WFP.
Picha: WFP/Martin Karimi
Duka la vyakula lililoanzishwa katika kijiji cha Kibagare, Nairobi, kutokana na msaada wa WFP.

 

Leah Wairimu ni mmoja wa wanufaika 68,000 wa msaada wa pesa wa WFP mjini Nairobi.
Photo: WFP/Martin Karimi
Leah Wairimu ni mmoja wa wanufaika 68,000 wa msaada wa pesa wa WFP mjini Nairobi.

 

Leah Wairimu anaendesha genge la vyakula huko Kibagare, kijiji kilicho karibu na mali isiyohamishika ya Loresho, katika mji mkuu wa Kenya wa Nairobi.  

Familia ya Leah ni moja kati ya watu 68,000 mjini Nairobi ambao wamepokea msaada wa pesa kutoka WFP. Kila mmoja akipata shilingi 4,000 za Kenya (Sawa na dola $ 37) kila mwezi kwa wiki 12. 

Mary, mpambaji na katika saluni kwenye kitongoji cha Kibagare mjini Nairobi, alipokea msaada wa fedha za WFP.
Picha: WFP/Martin Karimi
Mary, mpambaji na katika saluni kwenye kitongoji cha Kibagare mjini Nairobi, alipokea msaada wa fedha za WFP.

 

Katika siku yenye shughuli nyingi, angeuza  sahani kumi za chakula ambazo zinauzwa kwa shilingi 50 kila moja (chini ya nusu dola) alipokuwa akimiliki mgahawa. 

Lakini mwanzoni mwa janga la corona, migahawa yote ilifungwa. Mjane huyu anayelea watoto wa kiume watano, chanzo chake cha mapato kilipotea ghafla. 

“Nilitumia awamu mbili za kwanza za pesa kutoka WFP kwa chakula tu,” anasema, “Kisha, nikanunua mboga na matunda na nikafunguas genge dogo.” 

“Sikuruhusiwa kupika na kuhudumia wateja chakula kilicho tayari, lakini bado niliweza kuuza sukuma wiki, nyanya, dania na kupata faida kidogo." 

Hata hivyo awamu yake ya mwisho ya fedha toka WFP biashara yake ya mboga tayari ilikuwa ikifaidika. Biashara sasa inaendelea kupata faida na inampa mapato zaidi. 

Mary Wanjiku, ambaye alipokea msaada wa fedha mara nne kutoka kwa WFP, ni mpambaji katika kijiji cha Kibagare mjiini Nairobi.
Picha: WFP/Martin Karimi
Mary Wanjiku, ambaye alipokea msaada wa fedha mara nne kutoka kwa WFP, ni mpambaji katika kijiji cha Kibagare mjiini Nairobi.

 

Mbele kidogo kutoka kwenye genge la Leah, Mary ni mpambaji anayetoa huduma za ususi wa nywele za wanawake, kutengeneza kucha za mikono na miguu  na kurembesha zaidi nyuso.  

Mary ndiye muhimili pekee wa familia ya watu tisa; mumewe, watoto wao watatu na yatima wanne walioachwa na kaka yake.  

Ndani ya mwezi mmoja wa COVID-19 kugunduliwa nchini Kenya, biashara ya Mary iliporomoka na alilazimika kufunga duka lake. 

“Nilikuwa nikizama kwenye ankara. Pamoja na kupewa pesa mara nne, nilinunulia familia yangu chakula na kutenga kando kiasi kingine cha pesa ili kufufua saluni yangu ya nywele, ”anasema. “Biashara bado ipo katika hali mbaya lakini kuna matumaini. Sasa ninahudumia wateja wawili au watatu kwa wiki. ” 

Mary ana hamu ya kukuza biashara yake ya saluni ya nywele na anajua haswa anachohitaji kukifanya ili aweze kufanikiwa. 

“Tunachohitaji sana ni misaada kuturuhusu kukuza biashara zetu tofauti,” anasema. “Hiyo itatuletea mabadiliko ya kudumu.” 

Pamoja kusaidia wale wenye mahitaji  

Leah Wairimu, ambaye alipokea msaada wa fedha mara nne kutoka WFP, anatembea katika kitongoji cha Kibagare mjini Nairobi.
Picha: WFP/Martin Karimi
Leah Wairimu, ambaye alipokea msaada wa fedha mara nne kutoka WFP, anatembea katika kitongoji cha Kibagare mjini Nairobi.

 

Wengi, haswa vijana, wanataka fursa za kazi na biashara. 

“Tulipoanzakupokea fedha mjini Nairobi, tulifikiri ingekuwa ni mbio za haraka,” anasema Michael DeSisti, mkurugenzi wa mkoa katika ofisi ya usaidizi wa Kibinadamu ya USAID, Afrika Mashariki na Kati, ambao ni mshirika muhimu wa WFP. 

“Lakini kwa muda sio mrefu tuligundua kuwa tulikuwa kwenye mbio za muda mrefu. Kenya inahitaji msaada wa muda mrefu ili kukuza faida zilizopatikana hadi sasa. Hatuwezi kupoteza kasi ya sasa lazima tuendelee kutoa msaada.” 

Mpango unapomalizika, WFP itakuwa imetoa pesa za kuokoa maisha kwa karibu familia 95,000 au karibu watu 378,000 mijini Nairobi na Mombasa. 

Makazi yasiyo rasmi ya Huruma yaliyoko katika mji mkuu wa Kenya wa Nairobi.
Picha: WFP / Alessandro Abbonizio
Makazi yasiyo rasmi ya Huruma yaliyoko katika mji mkuu wa Kenya wa Nairobi.

 

“Hatungeweza kufanikiwa bila msaada kutoka kwa washirika kama USAID, wafadhili wetu wakubwa, na serikali za kitaifa na za kaunti zote Nairobi na Mombasa," anasema Lauren Landis, Mkurugenzi wa WFP nchini Kenya.  

“Lakini, idadi ya watu tuliowasaidia bado haitoshi  na watu, hawajaacha kulia. Watu wanatamani sana kujumuishwa katika msaada wa fedha, ila hatuwezi kuongeza idadi zaidi. ” 

WFP piainasaidia kutibu utapiamlo kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka 5, kina mama wajawazito na wanaonyonyesha, na wazee, kupitia vituo vya afya katika makazi yasiyokuwa rasmi ya Nairobi na Mombasa. 

“Tuko katika nafasi nzuri ya kutoa msaada wa kuokoa maisha na kupanua wigo wa huduma muhimu za jamii ili kuzilinda vyema familia hizi zilizo katika mazingira magumu, na tunagonga milango ya wafadhili wetu kutusaidia kufanikisha hili,” anaongeza Landis. 

Mradi wa utoaji wa msaada wa fedha wa WFP katika makazi yasiyo rasmi ya Kenya unafadhiliwa na USAID, nchi kama vile Finland, Poland na Sweden.