Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanawake na wasichana wakimbizi wahaha kupata taulo za kike DRC, UNHCR yawasaidia 

Janga la Corona limeathiri namna watu wanapitia hedhi salama.
©UNICEF/UNI328066/Nzenze
Janga la Corona limeathiri namna watu wanapitia hedhi salama.

Wanawake na wasichana wakimbizi wahaha kupata taulo za kike DRC, UNHCR yawasaidia 

Wahamiaji na Wakimbizi

Wanawake na wasichana wakimbizi waliotawanywa na machafuko nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo DRC wamekuwa wakiteseka kwa muda mrefu kupata taulo za kike kila mwezi kutokana na gharama huku wakijaribu kulinda uhai wao na kuhudumia familia zao baada ya kukimbia vita. Lakini sasa kwa msaada wa mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR wanaweza kujishonea taulo hizo na kujisitiri.

Hebu fikiria kuingia hedhi ukiwa ukimbizini , tena bila chochote na maisha yako yanategemea msaada wa wahisani kwa sababu ya vita vilivyokulazimisha kufungasha virago.

Natts tulikuwa tunatumikisha…… 

Joceline mmoja wa wanawake waliopitia madhila hayo akisema walilazimika kuhatarisha afya zao kwa kutumia matambara. Yuko katika eneo la Kitshanga DRC ambako ni makazi ya wakimbizi na watu wengi waliotawanywa na vita, “Ilikuwa shida hatukuwa tunapata taulo za kike, pesa nyingi tulipoteza kununua taulo hizo na hatuna pesa za kutosha kumudu gharama zake” 

Kupitia mradi wa UNHCR wa kusaidia wanawake na wasichana wakimbizi katika suala la afya ya hedhi, Joceline amekuwa miongoni mwa wanakikundi wa mradi huo wa kushona taulo za kike ambao umekuwa mkombozi mkubwa kwao ,Sasa tunatumia taulo hizi za kike ambazo tumezishona kwa mikono yetu, zina ubora mzuri na tunaweza kuzifua, tunaishukuru UNHCR kutusaidia sisi wanawake wakimbizi kwa kutuletea vyerehani na vifaa vingine , na sasa kazi yetu ni kushona taulo hizo ili kusaidia wanawake wengine” 

Kwa mujibu wa UNHCR imeanzisha mradi huo kwa sababu suala la hedhi katika maeneo yenye mizozo halipaswi kupuuzwa ni suala la afya, la dharura na ni huduma ya msingi.