Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
Jirani ya Delmas 32 katika mji mkuu wa Haiti, Port au Prince ni moja ya mahali ambapo kuna umasikini zaidi katika nchi za Karibea

Haiti: Ukosefu wa fedha unaweka rehani maisha ya watoto 86,000

World Bank/Dominic Chavez
Jirani ya Delmas 32 katika mji mkuu wa Haiti, Port au Prince ni moja ya mahali ambapo kuna umasikini zaidi katika nchi za Karibea

Haiti: Ukosefu wa fedha unaweka rehani maisha ya watoto 86,000

Msaada wa Kibinadamu

Idadi ya Watoto chini ya miaka 5 wanaougua utapiamlo mkali nchini Haiti inaweza kuongezeka zaidi ya mara mbili mwaka huu, ameonya Jean Gough mkurugenzi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Watoto – UNICEF katika ukanda wa Amerika kusini na karibiani, wakati akihitimisha ziara yake ya siku 7 katika nchi hiyo. 

Zaidi ya Watoto 86,000 nchini Haiti walio chini ya umri wa miaka 5 wanatabiriwa kupata utapiamlo mkali mwaka huu, ikilinganishwa na Watoto 41,000 mwaka jana, na wanaweza kupoteza maisha iwapo hawatapata msaada wa haraka. 

UNICEF imeshitushwa na ongezeko hilo la utapiamlo katika kipindi cha mwaka mmoja na imeonesha wasiwasi wake kutokana na upungufu wa chakula kilichotayari kama matibabu kwa wiki zijazo.

“Katika hospitali kadhaa nilizotembelea, nimehuzunika kuona Watoto wengi wakiteseka kutokana na utapiamlo, wengine hawatapona kama hawatapata matibabu kwa wakati” amesema Bi.Gough 
Watoto wanaoishi Haiti wapo kwenye ongezeko la hatari kubwa kutokana na mjumuisho wa mambo kadhaa ikiwemo kuzuka kwa vurugu, janga la Corona au COVID-19, ukosefu wa maji safi na salama, mazingira duni, pamoja na hali mbaya ya hewa. 

Katika kipindi cha janga la Corona, huduma za afya ziliathirika ikiwemo utoaji chanjo kwa Watoto. Kwa mujibu wa UNICEF asilimia 9.7 ya Watoto nchini Haiti hawajawahi kupata chanjo ya aina yeyote na asilimia 58 hawajapokea chanjo zote zinazotakiwa kwa Watoto. Na wale waliopokea chanjo zote, asilimia 42 wanaishi kwenye mazingira hatarishi ambako kuna uhaba wa huduma muhimu kwa Watoto na maeneo mengi yameathiriwa na vurugu. 

Mwaka 2020, UNICEF, serikali ya Haiti na washirika wake walitoa matibabu kwa Watoto 33,372. Kwa mwaka huu wa 2021, UNICEF ndani ya wiki chache kutoka sasa itaishiwa chakula chenye virutubisho kilicho tayari kinachotolewa kwa Watoto kutokana na uhaba wa fedha.

“UNICEF inahitaji kwa haraka jumla ya Dola za kimarekani Milioni 3 kwa ajili ya kununua mahitaji muhimu na dawa ili program ya kuwasaidia Watoto iweze kuendelea, iwapo fedha hizi hazitapatikana maelfu ya Watoto watakosa huduma wanazopatiwa kwa sasa za kuokoa maisha yao", amesisistiza Gough.

Kwa mwaka 2021, UNICEF inatafuta Dola za kimarekani milioni 48.9 ili kuweza kusaidia mahitaji ya kibinadamu yanayohitajika na watu milioni 1.5 nchini Haiti ambao kati yao zaidi ya 700,00 ni Watoto, hali ambayo imezidi kuwa mbaya kutoka na janga la COVID-19. Hadi sasa maombi haya ya msaada wa kibinadamu ni kama hayajasaidiwa kabisa