Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Poleni DRC kwa janga la mlipuko wa volkano Mlima Nyiragongo- Guterres

Anga la mji wa Goma jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC liligeuka jekundu baada ya volkano katika mlima Nyiragongo kulipuka taree 22 mwezi  mei mwaka 2021
MONUSCO/Tsok James Bot
Anga la mji wa Goma jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC liligeuka jekundu baada ya volkano katika mlima Nyiragongo kulipuka taree 22 mwezi mei mwaka 2021

Poleni DRC kwa janga la mlipuko wa volkano Mlima Nyiragongo- Guterres

Msaada wa Kibinadamu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza masikitiko yake kufuatia vifo, majeruhi na uharibifu wa mali uliosababishwa na mlipuko wa volkano katika mlima Nyiragongo, huko Goma jimbo la Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric akizungumza na waandishi wa habari hii leo jijini New York, Marekani amesema, “Katibu Mkuu anatuma salamu za rambirambi kwa familia za walioathiriwa na janga hilo, pamoja na serikali na wananchi wa DRC. Hofu yetu ni kwamba janga hili linakuja wakati kuna ongezeko tayari la mahitaji ya kibinadamu kwenye eneo hilo yanayochochewa na ukosefu wa usalama na hali ngumu ya kiuchumi.”

Bwana Dujarric amesema kwa mujibu wa wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, watu 13 wamekufa kutokana na mlipuko huo wa volkano katika mlima Nyiragongo na watu wengine wapatao 5,000 wamepoteza makazi yao.

Tweet URL

“Kama mnavyoweza kufikiria, idadi hiyo inaweza kubadilika kwa kuwa tunaendelea kupokea taarifa. Baada ya mlipuko, watu wengi walikimbilia huko Sake jimboni Kivu Kaskazini na wengine kuelekea Rwanda,” amesema Bwana Dujarric.

Kwa sasa barabara kati ya Rutshuru na Goma jimboni Kivu Kaskazini imefungwa, “na ni muhimu kutambua kuwa barabara hii ndio njia ya msingi ya kupeleka chakula mjini Goma. Njia za umeme na mabomba ya maji yameharibiwa na hivyo watu 500,00 hawana huduma ya maji na umeme.”

MONUSCO iko makini

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO nao uko makini kufuatilia hali ilivyo ambapo, “wakati wa mlipuko, helikopta ya MONUSCO  ikiwa imebeba wataalam wa volkano iliruka kwenye mazingira ya mlima Nyarugongo na viunga vyake kutathmini hali ilivyo hususan ya kusambaa kwa lava. “

Kwa mujibu wa Dujarric, lava ilisambaa hadi Munigi, ambako ni kilometa 5 kaskazini -mashariki mwa Goma ikiwa ni karibu na uwanja wa ndege ambao bado umefungwa.

Kufungwa kwa uwanja huo wa ndege kunakwamisha misafara ya watoa misaada ya kibinadamu na walinda amani.

Kwa sasa watu waliokimbia wameanza kurejea makwao ingawa mitetemo bado inaripotiwa kwenye eneo hilo, huku walinda amani wakijiandaa kuondoa takataka kwenye barabara kuu kuelekea Goma pindi hali itakaporuhusu.

Tathmini ya haraka inaendelea kufahamu mahitaji ya kibinadamu ili hatimaye kusaidia serikali katika kusambaza huduma za msingi kama vile maji, malazi, huduma za afya na kuunganisha familia, hasa wakati huu ambapo yaelezwa watoto makumi kadhaa wamepotezana na familia zao.