UNFPA inamuunga mkono Rais wa kwanza mwanamke Tanzania kusongesha usawa wa kijinsia
UNFPA inamuunga mkono Rais wa kwanza mwanamke Tanzania kusongesha usawa wa kijinsia
Ndoa za utotoni zimeendelea kuwaathiri wasichana wengi nchini Tanzania katika eneo la Afrika Mashariki, lakini kwa sasa juhudi mbalimbali zinazoungwa mkono na shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu duniani UNFPA zinatoa fursa kwa watoto na wbarubaru kupata msaada unaohitajika ili kuepuka mahusiano wasiyoyataka na yenye athari mbaya katika maisha yao.
Ilikuwa ni Ijumaa saa tisa adhuhuri kwa saa za Afrika Mashariki ambako Grace mshauri nasaha kwenye kituo cha kitaifa cha msaada kwa watoto nchini Tanzania alipopokea simu kutoka kwa mwalimu aliyejawa na hofu kwenye eneo la Msalala , mkoani Shinyanga nchini humo.
Mmoja wa wanafunzi wake mahiri Eliza , mwenye umri wa miaka 13, hakuwa ameenda shule siku hiyo kufuatia uvumi wa wasiwasi kuwa wazazi wake walikuwa wanakusudia kumuoza.
Aligundua kwamba walishapokea malipo ya kumuoza ambayo ni mahari kutoka kwa familia ya bwana harusi katika kijiji chao na mtu aliyechaguliwa kwa ajili ya Eliza alikuwa na umri wa miaka 35.
Katika ziara ya siku 2 nchini Tanzania iliyomalizika juma hili, Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la idadi ya watu duniani UNFPA, Dkt. Natalia Kanem, alikutana na washauri nasaha katika kituo hicho ya kitaifa cha msaada kwa watoto, kinachoendeshwa na C-Sema, shirika lisilo la kiserikali au NGO kwa kushirikiana na Serikali.
Huduma yao ya bure ya simu namba # 116, inayopatikana katika mitandao yote ya simu za rununu Tanzania bara na visiwani Zanzibar, inapokea simu karibu 3,500 kwa siku kutoka kwa wanawake na watoto walio katika hatari ya unyanyasaji, na kutoka kwa familia na wanajamii wanaoripoti unyanyasaji.
Washauri wa kujitolea waliofunzwa kama Neema huwapa wanawake na vijana msaada kwa saa 24 na kwa siku saba kwa wiki.
Washauri nasaha pia huwasiliana na mitandao ya msaada na mifumo ya ulinzi katika eneo la wapigaji simu ili kutoa msaada zaidi.
Hadithi ya Eliza ina mwisho mzuri. Kama matokeo ya uratibu wa Grace na mamlaka za serikali za mitaa na maafisa ustawi wa jamii wa wilaya huko Msalala, maafisa kutoka dawati la jinsia na watoto waliwatembelea wazazi wa Eliza na ndoa haikufungwa.
Jitihada za jamii nzima
Dkt. Kanem alitoa shukrani kwa C-Sema na washauri nasaha kwa kujitolea kwao kuendeleza usawa wa kijinsia na afya, haki na ustawi wa wanawake na vijana, pamoja na utumiaji wa majukwaa ya kidijitali na teknolojia mpya kufanikisha lengo hilo.
Licha ya hatua zilizopigwa na kujitolea kwa serikali ya Tanzania kukabiliana na pengo la usawa wa kijinsia na ubaguzi, kama ilivyoainishwa katika mipango ya kitaifa ya miaka mitano ya kukomesha ukatili dhidi ya wanawake na watoto, ukatili unabaki kuwa ukweli wa kila siku kwa wanawake wengi na wasichana barubaru.
UNFPA Tanzania inasaidia juhudi za kutokomeza unyanyasaji wa kijinsia na kuimarisha mifumo ya ulinzi kote nchini, ikiwa ni pamoja na kuanzisha nambari ya simu ya kitaifa ya watoto, Madawati ya polisi kushughulikia masula ya jinsia na watoto, na kuwa na kituo kituo kimoja kinachoshughulikia changamoto hizo.
Vituo vya jamii, ambako wanawake wanasaidiana na kuongoza katika juhudi za kumaliza unyanyasaji katika jamii zao, pia vimeanzishwa.
Kuwawezesha wanaume na wavulana kama chachu ya mabadiliko
Jitihada za kumaliza ukatili hazijalenga tu kuwawezesha wanawake na wasichana. Wanaume na wavulana, na viongozi wa jadi na jamii, pia wamejumuishwa katika mazungumzo kwa kutambua jukumu lao na mchango wao kwa usawa wa kijinsia.
Kupitia mkakati wa ufikiaji mkubwa wa jamii, washirika wa UNFPA wanahimiza majadiliano juu ya maoni ya mfumo dume na njia nzuri za kuunga mkono haki za wanawake na wasichana.
Kuwashirikisha wanaume ili kuwawajibisha wanaume wengine ni muhimu katika kuunda msingi wa usawa zaidi na hawapaswi kuachwa nyuma, amesisityiza Dkt. Kanem. "Kila msichana na mvulana anapaswa kuthaminiwa na anapaswa kufundishwa kuwa kuelezea haki yake na uwezeshawji wake havipaswi kufikiriwa kuwa vinalenga kulenga kuwazidi nguvu wengine."
Kusaidia juhudi zinazoongozwa na serikali
Wakati wa ziara yake nchini Tanzania, Dkt Kanem alikutana na Rais wa kwanza mwanamke wa nchi hiyo, mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ambaye alielezea dhamira ya Serikali ya Tanzania ya kutokomeza vifo vya mama na mtoto vinavyoweza kuzuilika, unyanyasaji wa kijinsia na mila potofu, ikiwemo ukeketaji wa wanawake. .
Dk Kanem amepongeza uongozi wa serikali na kusisitiza msaada wa UNFPA kwa Tanzania ili kufikia malengo ya maendeleo na ukuaji wa uchumi na kijamii ulio na nguvu zaidi, ukiwa na lengo la kutokumuacha mtu yeyote nyuma.