Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mlipuko wa 12 wa Ebola Kivu Kaskazini umetokomezwa - WHO 

Mhudumu wa afya akimchanja dhidi ya Ebola, mwanaume mjini Beni, mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC.
World Bank/Vincent Tremeau
Mhudumu wa afya akimchanja dhidi ya Ebola, mwanaume mjini Beni, mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC.

Mlipuko wa 12 wa Ebola Kivu Kaskazini umetokomezwa - WHO 

Afya

Shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO hii leo kupitia taarifa iliyotolewa mjini Brazzaville Congo na  Kinshasa, DRC, limetangaza kumalizika kwa mlipuko wa 12 wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, miezi mitatu tu baada ya mgonjwa wa kwanza kuripotiwa Kivu Kaskazini.  

WHO imepongeza mamlaka ya afya ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na wafanyakazi wa afya kwa hatua yao ya haraka ambazo zinatona na uzoefu wa hapo awali wa nchi hiyo katika kukabiliana na milipuko ya Ebola. Mlipuko huu ni wa nne kwa nchi hiyo katika kipindi cha chini ya miaka mitatu. 

Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt Tedros Adhanom Ghebreyesus akiwa mjini Geneva, Uswisi, amewapongeza wote waliohusika katika kumaliza mlipuko wa 12 wa Ebola mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, na kusisitiza hitaji la kuendelea kuwa macho ili kuzuia kurudi kwa ugonjwa huo na katika kuwa na changamoto zingine za kiafya. 

"Tangazo la leo la kumaliza mlipuko wa hivi karibuni wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni ushahidi wa taaluma, kujitolea, na ushirikiano na mamia ya mashujaa wa kweli wa afya, haswa wajibu wa Kongo. Shirika la Afya Ulimwenguni limejitolea kusaidia mamlaka za kitaifa na za mitaa, na watu wa Kivu Kaskazini, kuzuia kurudi kwa virusi hivi hatari na kukuza afya na ustawi wa jamii zote zilizo hatarini." Amesema Dkt Tedros. 

Mlipuko wa Ebola ulioibuka tena mnamo Februari ulikuja miezi tisa baada ya mlipuko mwingine katika jimbo hilo hilo kutangazwa kuwa umekwisha.  

Aidha, Dkt Tedros amesema kurudi kwa virusi mapema mwaka huu kunasisitiza vitisho vya afya vinavyoendelea ambavyo watu huko Kivu Kaskazini wanakabiliwa, na hitaji la wote wanaohusika katika kukuza na kulinda afya ya umma kukaa macho mbele ya Ebola, na vile vile COVID-19 , surua, kipindupindu na changamoto zingine zinazokabili jamii, zote zikiwa katika hali ngumu ya tabianchi na vurugu. 

Katika mlipuko wa hivi karibuni, ambao sasa umetangazwa kumalizika, visa vya maambukizi 11 vilivyothibitishwa, pamoja na kisa kimoja ambacho kilihisiwa, vifo sita na waliopona sita vilirekodiwa katika maeneo manne ya afya tangu 7 Februari.  

WHO ilikuwa na wataalam takribani 60 nchini DRC na mara tu mlipuko ulipotangazwa ilisaidia wafanyakazi wa nchini humo kutafuta watu waliokutana na wagonjwa, kutoa matibabu, kushirikisha jamii na chanjo kwa takribani watu 2000 walio katika hatari kubwa, pamoja na wafanyakazi wa mstari wa mbele zaidi ya 500. 

WHO imeongeza kusema kuwa wakati mlipuko huu wa hivi karibuni umekwisha, kuna haja ya kuendelea kuwa macho na kudumisha mfumo thabiti wa ufuatiliaji kwani uwezekano wa kutokea tena unawezekana katika miezi ijayo. Ni muhimu vile vile kuendelea kuboresha kinga na udhibiti wa maambukizo katika vituo vya afya ili kuzuia magonjwa yote ya kuambukiza, na kuendelea kusaidia waathirika wa Ebola kupitia programu za kujitolea za ukarabati. Vitendo kama hivyo vinapaswa kuungwa mkono na juhudi za kujitolea za kuboresha changamoto zinazoendelea zinazosababishwa na ukosefu wa usalama na vurugu za silaha katika mkoa wa Kivu Kaskazini.