Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mashirika ya UN yaendelea kufikisha nuru kwa wakimbizi huko Ituri DRC 

Wanawake wakiwa wamekusanyika katika kituo cha kugawa chakula cha Nyanzale Kivu Kaskazini DRC. Kituo hicho kinawalenga kwa msaada familia zisizojiweza na zilizo hatarini
OCHA/Ivo Brandau
Wanawake wakiwa wamekusanyika katika kituo cha kugawa chakula cha Nyanzale Kivu Kaskazini DRC. Kituo hicho kinawalenga kwa msaada familia zisizojiweza na zilizo hatarini

Mashirika ya UN yaendelea kufikisha nuru kwa wakimbizi huko Ituri DRC 

Msaada wa Kibinadamu

Katika jimbo la Ituri nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Umoja wa Mataifa kupitia mashirika yake umeendelea kusambaza misaada kwa wakimbizi wa ndani ambao walilazimika kukimbia makwao na kuacha kila kitu na hivi sasa wanaishi kwenye kambi za wakimbizi hususan katika eneo la Pinga jimboni humo. Misaada hiyo imekuwa jawabu kwa wakimbizi ugenini.

Msafarwa wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF ukielekea eneo la Pinga jimboni Ituri ukisindikizwa na walinda amani waUmoja wa Mataifa nchini  DRC, MONUSCO

Shehena ni vifaa kama vile vikasha vya kujisafi na nguo wakati shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa, WFP lenyewe linagawa vyakula. 

Msafara huu ni jawabu kwa wakimbzi kama vile Bauma Riziki, ambaye anasimulia masahibu yake,“Wanamgambo walipofika kijijini kwetu, walifyatua risasi, wakati tunajaribu kukimbia, mume wangu alipigwa risasi na kufa papo hapo. Nilikimbilia msituni na watoto wangu, na kisha tukafika hapa. Tulipokimbia tuliacha kila kitu. Nilikuja na gauni langu hili moja na kikombe kile pale. Tulipoteza kila kitu.” 

Kuwasili kwa malori yenye shehena kunaleta nuru kwa wakazi ambapo baada ya mizigo kushushwa wakimbizi wanaelimishwa kuhusu kifaa kimoja baada ya kingine. 

Bauma anasema, “Tulipofika hapa, watu waliona jinsi ambavyo nilikuwa nahaha kulea watoto wangu  na walianza kunipatia unga ili niwapikie watoto uji. Ni watu niliokutana nao hapa kijijini ndio walinisaidia.” 

Kisha wakaanza kuitwa mmoja baada ya mwingine ili kukabidhiwa shehena zao, na ikafikia zamu ya Bauma! “Hatukuwa tumepokea msaada wowote hadi leo hii. Vifaa hivi vitanisaidia sana mimi na watoto wangu.” 

Baada ya kupokea vifaa hivyo, Bauma anarejea nyumbani na angalau tabasamu sasa akisema “Maisha yatakuwa angalau nafuu kidogo baada ya kupata vifaa hivi. Sasa naweza kulisha mwenyewe watoto wangu,” 

Kwa mujibu wa Hye Sung, mtaalamu wa masuala ya dharura wa UNICEF nchini DRC, msaada huu na ule wa WFP umesaidia wakimbizi kuweza angalau kujipatia chakula cha kupika huku akisema “kwa kweli inakatisha tamaa, siyo tu kwa UNICEF bali pia kwa wannachi ambao wamekuwa wanasubiri msaada na huu si msaada ambao wanapaswa kusubiri bali wanahitaji zaidi msaada hivi sasa.”