Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ujumuishaji wa watu wenye ulemavu ni haki ya msingi ya binadamu:Guterres

Kijana barubaru akitumia teknolojia ya maadishi hadi sauti katika shule ya elimu kwa watu wanaoishi na ulemavu Kuala Lumpur, Malaysia.
UNICEF/Pirozzi
Kijana barubaru akitumia teknolojia ya maadishi hadi sauti katika shule ya elimu kwa watu wanaoishi na ulemavu Kuala Lumpur, Malaysia.

Ujumuishaji wa watu wenye ulemavu ni haki ya msingi ya binadamu:Guterres

Masuala ya UM

Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa amesema wakati dunia ikijikwamua kutoka kwenye janga la COVID-19 ni lazima kuhakikisha kwamba matarajio na haki za watu wenye ulemavu zinajumuishwa na hilo litatimia tu endapo watu hao watashirikishwa na kuwakilishwa ipasavyo. 

Kupitia ujumbe wake wa siku hii Antonio Guterres amesema ujumuishwaji huo ni haki ya msingi ya binadamu na kwamba, “Tunapopambana kutimiza haki hiyo tunaisogeza karibu dunia katika kutimiza maadili na misingi ya katiba ya Umoja wa Mataifa.” 

Ameongeza kuwa ndio maana katika mwanzo wa uongozi wake aliagiza kufanyika tathimini ya ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu katika Umoja wa Mataifa na hasa kuangalia mapengo yaliyopo na kisha mwaka jana akazindua mkakati maalum wa Umoja wa Mataifa wa ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu. 

“Mkakati huo ni wa kuchukua hatua za kuinua viwango vya utendaji wetu kuhusu ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu katika mfumo mzima na hatua za kuleta mabadiliko tunayoyahitaji. Mwaka mmoja baadaye tunaona kwamba mkakati huo umeleta hatua chanya lakini bado kuna safari ndefu.” 

Katubu Mkuu amesisitiza kwamba anataka Umoja wa Mataifa uwe mfano na mwajiri ambaye ni chaguo la watu wenye ulemavu  na pia mtambuaji na msongeshjaji mbele wa haki za watu hao kwani 

“Lengo letu liko bayana la kuwa na dunia ambayo watu wote wakiwemo watu wenye ulemaavu wanafurahia fursa sawa, wana sauti katika kufanya maamuzi na kufaidika kutokana na maisha ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni  

Siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu huadhimishwa kila mwaka Desemba tatu na maudhui ya mwaka huu ni "kujijenga vyema upya kuelekea dunia endelevu yenye ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu, baada ya janga la COVID-19."