Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Janga la nzige laendelea kuzusha zahma kubwa kwa wakulima na wafugaji Yemen:FAO 

Nzige wa jangwani ambao wanaendelea kuzaliana nchini Yemen.
© FAO/Haji Dirir
Nzige wa jangwani ambao wanaendelea kuzaliana nchini Yemen.

Janga la nzige laendelea kuzusha zahma kubwa kwa wakulima na wafugaji Yemen:FAO 

Msaada wa Kibinadamu

Maisha ya wakulima na wafanyakazi yameendelea kupata pigo kubwa kutokana na janga linaloendelea la nzige nchini Yemen ambao wamesambaratisha mazao, malisho ya mifugo na kuongeza shinikizo kwa maelfu ya watu ambao tayari wamechoshwa na miaka ya vita vinavyoendelea nchini humo limesema shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa FAO.

Katika Kijiji cha Hareeb jimbo la Ma’rin nchini Yemen mkulima na mfugaji  Musaeed Mubarak Ali Al-Gunaimi akitembelea shamba lake kuangalia uharibifu uliofanywa na nzige hao wa jangwani anasema wameshambulia mazao yote ya wakulima kuanzia matunda, vitunguu, ufuta, mpunga na hata mitende na kusababisha hasara kubwa kwao. Na kana kwamba hilo halitoshi ,“Makundi ya nzige hao yameshambulia mashamba na kumaliza mazao yote na sasa kilichosalia yatakula chakula cha mifugo ambacho tunatumia kulisha kondoo wetu” 

FAO inasema imekuwa ikiisaidia wizara ya kilimo na umwagiliaji ya Yemen kupambana na nzige hao wa jangwani kwa operesheni mbalimbali ikiwemo za kiuifundi na mafunzo kwa timu za mashinani. Lakini maeneo yaliyoathirika ni mengi. Hussain Mohamed Abdullah Al-Zubaid ni mkulima kutoka jimbo la Tarim anasema,“Nzige wamekula kila kitu ndani ya siku nne na hawakuacha chochote isipokuwa vijiti” 

Msaada wa FAO ni pamoja na zaidi ya lita 14,850 za dawa za kuulia wadudu na mafunzo kwa watu 393 ambao watahusiska na masuala ya afya, usalama na mazingira wakikabiliana na nzige hao. Msaada ambao umepokelewa kwa mikono miwili na wakulima na wafugaji wa Yemen kama anavyosema mkurugenzi mkuu wa kituo cha ulinzi wa mazao na wkulima Yasir Mohammed Saleh Ali,“Tumeathirika sana kwa kukosa uwezekano na msaada wa fedha, hata hivyo tunaishukuru FAO kwa juhudi zake na kituo cha ulinzi wa mazao na wakulima kwa kuwezesha zoezi hili. Mungu akijalia tutaanza jukumu  na kusaidia tuwezavyo. Bado tunahitaji timu ya watu zaidi kwa sababu hatujaweza kushugfhulikia eneo lote sababu tuna magari mawili tu hapa na moja lni a kufanya ukaguzi.” 

Kwa mujibu wa FAO kutokana na vita sio maeneo yote yanayoweza kufikiwa na msaada kwa sababu ya usalama hali ambayo inawapa nzige fursa ya kuzaliana na kuongezeka na hivyo kuongeza shinikizo kwa wakulima na wafugaji  nchini humo.