Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uchaguzi mwema Tanzania-UN 

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres
UN News
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres

Uchaguzi mwema Tanzania-UN 

Amani na Usalama

Wakati watanzania wakijiandaa kushiriki uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika tarehe 28 Oktoba, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito kwa wadau wote wa kitaifa kuhakikisha kuwa upigaji kura unafanyika kwa umoja na kwa amani.  

Katibu Mkuu Guterres katika taarifa aliyoitoa hii leo kupitia msemaji wake mjini New York Marekani, amesema kuwa mchakato wa pamoja wa uchaguzi na ushiriki mpana wa vyama vya siasa na wagombea wao, hasa wanawake, unabakia kuwa muhimu kwa kulinda maendeleo yaliyofanywa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha utulivu, demokrasia na maendeleo endelevu.  

“Katibu Mkuu anawataka viongozi wote wa kisiasa na wafuasi wao kushiriki zoezi hili kwa amani na kujiepusha na vurugu. Anatoa wito zaidi kwa mamlaka kuweka mazingira salama na ambayo yataruhusu watanzania kushiriki haki zao za kiraia na kisiasa.” Umesema ujumbe huo.  

Aidha Katibu Mkuu Guterres amesisitiza ahadi ya Umoja wa Mataifa kuunga mkono juhudi za Tanzania kukuza maendeleo endelevu na kujenga mustakabali mzuri. 

Tanzania inategemea kufanya uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani keshokutwa Jumatano, ambapo rais wa sasa wa nchi hiyo John Pombe Magufuli anawania kuongoza muhula wa pili katika kinyang’anyiro ambacho kinashirikisha vyama vingine vya upinzani ambavyo navyo vimenuia kuchukua uongozi wa nchi hiyo iliyoko Afrika Mashariki.