Skip to main content

UNDP yaleta matumaini kwa wakulima wa Habanero nchini Tanzania

Mashamba haya ya mfano ya kilimo cha pilipili aina ya Habanero ni sehemu ya miradi ya UNDP Tanzania ya kuinua kiuchumi wanawake na vijana.
UNDP Tanzania/Sawiche Wamunza
Mashamba haya ya mfano ya kilimo cha pilipili aina ya Habanero ni sehemu ya miradi ya UNDP Tanzania ya kuinua kiuchumi wanawake na vijana.

UNDP yaleta matumaini kwa wakulima wa Habanero nchini Tanzania

Wanawake

Nchini Tanzania, shirika la mpango wa maendeleo la Umoja wa Mataifa, UNDP limewezesha chama cha wakulima wa mboga na matunda nchini humo, TAHA kusaidia wanachama wake kulima kilimo bora cha mazao hayo kupitia mashamba ya mfano na ya kisasa na sasa wanapata masoko nchi za nje.

Ujumbe wa UNDP uliotembelea mashamba ya TAHA mkoani Kilimanjaro na Arusha ulishuhudia mashamba yakiwa yameshamiri na wakulima wakiwa na matumaini siyo tu ya kuvuna mazao bora bali pia kupanua kilimo chao.

Miongoni mwa wanufaika ni Betty Gadson Mrema wa kikundi cha Umwagiliaji Uchira kinachomiliki shamba la mfano la Pilipili aina ya Habanero kwa ajili ya kuuzwa nje ya nchi.

Bi. Mrema anasema, “kikundi chetu kina wanachama 30 na tuliamua kuunda kikundi kwa kuwa ukiwa na kikundi kuna faida nyingi kama vile mnapata  watu wa kuwaelekeza, maafisa ugani wanakuwa karibu na sisi, tunapata elimu, wanatufundisha. Pia wametueleza watatupatia wafadhili na udhamini.”

Soundcloud

Alipoulizwa ni kwa nini waliamua kulima pilipili na si kilimo kingine, mwanachama huyo wa kikundi cha Umwagiliaji Uchira kinachoratibiwa na TAHA amesema, “tuliamua kulima pilipili kwa sababu tuliona ni  klimo kizuri na kina soko, tuliambiwa soko lake liko nje kwa hiyo kinakuwa ni cha uhakika. Hii ni tofauti na kilimo kingine ambacho tulikuwa tunalima. Tulikuwa tunalima na mazao na yanabakia shambani na hakuna mtu wa kununua.”

Kwa kikundi hiki, kilimo cha sasa cha pilipili aina ya Habanero ni cha kwanza, lakini awali walilima  la uhakika. Hii ni tofauti na kilimo cha mazao mengine kama nyanya, vitunguu na pilipili mbuzi ambazo wameshavuna na kwamba, “sasa tumeingia kwenye kilimo hiki tulichoambiwa ni cha mkataba na kina faida kwa sababu tayari tuna mahali pa kuuza, tofauti na kile cha kwanza ambacho kilikuwa ni cha kutafuta soko, kwa hiyo hatukupata faida kulingana na masoko. Sasa tuna uhakika kuwa tukivuna pilipili tuna mahali pa kupeleka.”

Ujumbe wa UNDP Tanzania ukiwa na wanakikundi wa shamba la mfano la kilimo cha pilipili aina za Habanero kwa ajili ya soko la nje, mkoani Kilimanjaro.
UNDP Tanzania/Sawiche Wamunza
Ujumbe wa UNDP Tanzania ukiwa na wanakikundi wa shamba la mfano la kilimo cha pilipili aina za Habanero kwa ajili ya soko la nje, mkoani Kilimanjaro.

Kwa nini Habanero Kata ya KAHE mkoani Kilimanjaro?

Enock Florian Ngowi ni bwana shamba wa TAHA mkoani Kilimanjaro ambaye anasema kuwa walichagua eneo lenye joto katika kijiji cha Kyomu  Kata ya Kahe kwa kuwa hali hiyo ya hewa ni murua kwa kilimo cha pilipili aina ya Habanero.

“Pilipili zinakomaa baada ya miezi miwili na nusu tangu kuhamishiwa shambani kutoka kwenye kitalu. Na unaweza kuvuna kwa muda mwaka mmoja hadi mwaka mmoja na nusu. Na kila wiki unaweza kuvuna pilipili,” amesema Bwana Ngowi.

UNDP Tanzania inatekeleza mradi huo wa kilimo endelevu ikilenga vijana na wanawake.

Maeneo ambayo tayari yananufaika ni Arumeru mkoani Arusha, Moshi vijijini, Siha na Same mkoani Kilimanjaro, Bunda mkoani Mara, Busega mkoani Simiyu na wilaya za Njombe, Wanging’ombe na Ludewa mkoani Njombe.

Kwa sasa TAHA kupitia msaada wa UNDP inajenga vituo vinne huko Same mkoani Kilimanjaro.