Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nilianzisha PsychHealth kuziba pengo la huduma za afya ya akili Zambia:Chiwele

Siku ya kimataifa ya afya ya akili  inalenga katika kukuza uelewa wa kiwango cha visa vya kujiua na jukumu la kila mmoja katika kuzuia
WHO
Siku ya kimataifa ya afya ya akili inalenga katika kukuza uelewa wa kiwango cha visa vya kujiua na jukumu la kila mmoja katika kuzuia

Nilianzisha PsychHealth kuziba pengo la huduma za afya ya akili Zambia:Chiwele

Afya

Kutana na Kayumba Chiwele mwanaharakati wa masuala ya afya ya akili nchini Zambia na pia mshindi wa tuzo ya Benki ya Dunia ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs katika kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika iliyotolewa mwishoni mwa wiki. Yeye na shirika alilolianzisha la PsychHealth wanapigia upatu upatikanaji wa huduma za afya ya akili hasa wakati huu wa janga la corona au CIVID-19.

 

Bi. Kayumba Chiwele huyo akisema suala la afya ya akili Zambia linahusiana na unyanyapaa mkubwa, mwiko kulizungumzia, wataalam ni wachache na hata huduma zake ni adimu, kwani mji mzima wa Lusaka ambao ni mji mkuu wa taifa hilo kuna hospitali moja tu ya afya ya akili, suala lililomsukuma kuzindua huduma ya kwanza kabisa ya afya ya akili inayopatikana kwa saa 24 kupitia mtandao nchini humo, “hivyo tukaanzisha PsychHealth Zambia sisi ni shirika linalotoa huduma ya afya ya akili , kwa sasa ni Lusaka peke yake lakini tunatumai kwenda nchi nzima “ 

Pia lengo lao ni kuelimisha na kuchagiza jamii nzima kufahamu kuhusu sula la afya ya akili, na walianza kama timu ya watu wawili wakiwalenga zaidi wale wenye msongo wa mawazo, shinikizo na walio katika hatari za ukatili hususan wanawake  na wasichana. Na juhudi zao zinazaa matunda kwani anasema, “shirika letu sasa limeanza kutambulika na watu wanathamini kazi yetu kwa sababu kila mtu alikuwa anajua tu kuhusu hospitali ya wagonjwa wa akili ya Chainama, ndipo tukajitokeza, na pia ni shirika linaloendeshwa na vijana, na tangu hapo tumepokea ushirikiano na msaada kutoka wizara ya afya na sasa tunafanyanao kazi pamoja na makundi mengine kujaribu kuziba mapengo katika huduma ya afya ya akili.” 

Dhamira yake ni kumfika kila mahali Zambia katika majimbo yote 10 ya nchi hiyo. Na mchango wake haujatambulika Zambia pekee hadi Benki ya Dunia ambao wamemtunuku tuzo ya SDGs kwa jitihada hizo.