Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hakuna nchi hata moja inaweza peke yake kumudu janga kama hili la COVID-19

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya akihutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa UNGA75 kwa njia ya video.
UN Photo/Evan Schneider
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya akihutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa UNGA75 kwa njia ya video.

Hakuna nchi hata moja inaweza peke yake kumudu janga kama hili la COVID-19

Afya

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya hii leo akihutubia mjadala wa wazi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa njia ya vdeo iliyorekodiwa kutokana na janga la virusi vya corona kutoruhusiu viongozi wa dunia kukutana New York Marekani kama ilivyo ada ya kila mwaka, ameueleza ulimwengu kuwa ugonjwa wa COVID-19 linapaswa kutoa msukumo mpya, “kwa juhudi zetu za pamoja za kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.” Na hakuna nchi ambayo peke yake inaweza kumudu janga kubwa la kiwango cha COVID-19. 

Rais Kenyatta ameeleza kuwa janga hili la kimataifa limeongeza zaidi hali iliyokuwepo ya kukosekana kwa usawa, na kuziathiri zaidi jamii maskini na zilizoko hatarini na kwa hivyo kutokana na kuonekana umuhimu wa ushirikiano kuna uhitaji wa haraka kuboresha utayari katika eneo la usimamizi wa majanga ya kimataifa.  

Kenyatta akizungumzia hatua ambazo Kenya ilizichukua ili kukabiliana na janga la corona amesema timu ya taifa 

Timu ya kitaifa kuhusu COVID19 iko ili kuhakikisha kuna hatua zinazofaa na kwamba kama nchi wamebadilisha na kupanua mifumo ya kitaifa na kaunti katika suala la kushughulikia afya. Hatua  ambazo wamechukua zinawalenga wazee na watu wengine walio katika mazingira hatarishi, wasio na ajira na vijana.  

“Tumetambua pia kuwa janga hili limetoa changamoto za usawa wa kijinsia na zaidi unyanyasaji wa kijinsia.” Amebainisha Rais Kenyatta.  

Aidha Bwana Kenyatta amesema, “tumeanzisha hatua za kifedha na ushuru ili kuweka uchumi na biashara vyema. Na kama ilivyo wengine, Kenya imechukua hatua za afya ya jamii kama vile kusitisha kwa usafiri, umbali kati ya mt una mtu, kuvaa barakoa na kuboresha usafi kwa wote.”   

Katika ngazi ya bara, Rais Kenyatta amesema kwa kufanya kazi na Muungano wa Afrika, yeye mwenyewe amehusika katika kuweka hatua za pamoja za bara akiwa pamoja na wakuu wengine wa mataifa na serikali ambao ni wanachama wa Muungano wa Afrika. 

“Tulipitisha mkakati wa kupunguza COVID-19 katika bara la Afrika, ambao umekuwa na mafanikio makubwa katika kuratibu juhudi za bara kuzuia vifo kutokana na COVID-19; pamoja na kupunguza kuvurugwa kwa kijamii na kiuchumi.” Amesema Uhuru Kenyatta.  

Kwa msingi huo Rais Kenyatta akasisitiza akisema, “kile ambacho tumejifunza katika miezi sita iliyopita, hakuna nchi na narudia, hakuna nchi inayoweza kushughulikia janga la kiwango hiki, peke yake. Imetubidi kufanya kazi kwa pamoja ili kurejea katika hali nzuri.” 

Na kisha Bwana Kenyatta akatoa wito kwa jumuiya kimtaifa kuongeza ushirikiano na usaidizi kwa nchi zinazoendelea katika hali hatarishi ili kuimarisha uchumiwao na mifumo yao ya afya na kufikia afya kwa wote kama ilivyotazamiwa tamko la kisiasa la mwaka 2019.