Maelfu ya waathirika wa mafuriko Sudan Kusini wapokea msaada wa WFP

Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula WFP , limefikisha msaada wa chakula uhaohitajika haraka kwa maelfu ya watu walioathirika na mafuriko Jonglei Sudan Kusini ili kuwaepusha na janga la njaa.
Kwa mujibu wa shirika hilo mvua kubwa na mafuriko yanayoendelea kwenye jimbo la Jonglei Mashariki mwa Sudan Kusini vimewatawanya zaidi ya watu 120,000 ambao wamezikimbia nyumba zao na kusaka hifadhi kwenye mji wa karibu wa Bor.
Hivi sasa WFP inazifikia familia zilizo hatarini zaidi kwa msaada wa haraka wa chakula na lishe ikiwemo ya watoto. Shirika hilo linasema kabla ya mafuriko haya machafuko ya mara kwa mara kwenye jimbo la Jonglei na viunga vyake yalizitawanya jamii nyingi, na kuzipokonya maisha yao ikiwa ni pamoja na kuwatumbukiza katika janga la njaa na umasikini.
Mkurugenzi wa WFP nchini Sudan Kusini Matthew Hollingworth yuko katika jimbo hilo la Jonglei ili kutathimini hali halisi ya kibinadamu.
Katika ziara hiyo pia atakutana na familia za Sudan Kusini ambazo zimepoteza kila kitu ikiwemo nyumba zao na uwezo wa kujikimu kimaisha na pia waliopoteza wapendwa wao kutokana na mafuriko hayo na machafuko yanayoendelea Jonglei.