Walinda a.mani wa Umoja wa Mataifa wachangia damu Lebanon
Walinda a.mani wa Umoja wa Mataifa wachangia damu Lebanon
Umoja wa Mataifa kupitia mashirika yake na wadau, wameendelea kutoa misaada kwa waathirika wa mlipuko uliotokea Agosti 4 katika mji mkuu wa Lebanon Beirut. Takribani walinda amani 100, wanajeshi na raia, wamejitolea kuchangia damu kwani bado uhitaji ni mkubwa.
Maafisa wa shirika la msalaba mwekundu wa Lebanon wanaonekana wakishusha na kuunganisha vifaa katika kiliniki ya ikosi cha mpito cha Umoja wa Mataifa nchini Lebanon, UNIFIL, kwa ajili ya kukusanya damu.
Maafisa 96 wa UNIFIL kwa kushirikiana na shirika la msalaba mwekundu la Lebanon wamechangia damu katika hospitali ya UNIFIL iliyoko Naquura, kusini mwa Lebanon.
Uchangiaji wa damu imekuwa ni sehemu ya juhudi za UNIFIL kusaidia raia wa Lebanon kutokanana na madhara yaliyoachwa na mlipuko ambao pia uliharibu meli ya UNIFIL iliyokuwa imetia nanga katika bandari ya Beirut na hivyo kujeruhi maafisa 23 wa UNIFIL.
Celine Atimeh, ni Muuguzi Mkuu katika Hospitali ya makao makuu ya UNIFIL anasema, “Tunafanya kampeni ya kuchangia damu kwa kushirikiana na shirika la msalaba mwekundu la Lebanon. Wazo na mkakati vilikuja kutoka kwa viongozi wa juu wa UNIFIL siku ya pili baada ya mlipuko wa Beirut na hii ndiyo sababu UNIFL ikataka kushiriki katika kuwasaidia watu wa Lebanon.”
Celine anaongeza kuwa wanapokea maombi mengi ya mchango wa damu kutoka katika hospitali za mjini Beirut. Kwa hivyo nwakawahusisha shirika la msalaba mwekundu ambao walionesha utayari kwenda Naqoura na kufanya kampeni hii ya uchangiaji damu.
Mmoja wa wachangiaji ni Eugene Friel, Afisa mwandamizi wa masuala ya siasa katika UNIFIL anasema, “Niko hapa kuchangia damu leo ili kusaidia waathirika wa mkasa wa Agosti 4 Beirut. Ni muhimu kwamba tufanye kila tuwezalo katika kipindi hiki kigumu kwa wote waliohusika, na kitendo rahisi cha kutoa kiasi kidogo cha damu kinaweza kwenda mbali zaidi na kuokoa maisha ya mtu.”
Mchangiaji mwingine wa damu ni Kapteni Jennifer Barrientos, mlinda amani kutoka Guatemala ambaye anaona ni muhimu sana kusaidina hususani katika kipindi kigumu kama hiki katika Lebanon. “Kama mlinda amani wa UNIFIL, ni muhimu kuweza kusaidia watu wa Lebanon na raia wake. Na njia moja ya kutoa punji yetu ya mchanga ni kwa kutoa damu ambayo ndiyo walebanon wanaihitaji haraka hivi sasa.”