Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuendeleza huduma za msingi Sudan Kusini ni muhimu katika mapambano ya COVID-19:UNICEF

Mtoto akipokea dawa za TB nchini Sudan Kusini kwa msaada wa Global Fund kupambana na VVU,TB na Malaria
UNDP South Sudan/Brian Sokol
Mtoto akipokea dawa za TB nchini Sudan Kusini kwa msaada wa Global Fund kupambana na VVU,TB na Malaria

Kuendeleza huduma za msingi Sudan Kusini ni muhimu katika mapambano ya COVID-19:UNICEF

Afya

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, limesema muendelezo wa huduma za msingi zikiwemo chanjo kwa watoto Sudan Kusini ni muhimu sana katika vita dhidi ya janga la corona au COVID-19 na maradhi mengine.

Kwa mujibu wa UNICEF, nchini  Sudan Kusini asilimia 60 ya watu wanakosa huduma ya maji safi, watoto milioni 1.3 wataugua utapiamlo na kiwango cha chanjo hivi sasa ni asilimia 40 tu.  

Shirika hilo limeonya kwamba watoto wengi wako hatarini na kushughulikia mahitaji yao ya msingi ni muhimu sana ili kuwawezesha kuishi wakati huu wa janga la COVID-19, kwani hatua za kupambana na gonjwa hilo zimepunguza fursa za huduma na kuwema uhai wao njiapanda. 

Shirika hilo linasema watoto wengi wanakosa chanjo za msingi,  shule zimefungwa na wengi wako katika hatari ya ukatili na unyanyasaji. 

Licha ya changamoto hizo UNICEF na wadau wake wanajitahidi kuendelea kutoa huduma za kuokoa maisha na hadi kufikia sasa mwaka huu pekee watoto 292,000 wamepatiwa chanjo ya surau na milioni 1.6 wamepewa matone ya vitamin A. 

Mbali ya chanjo, UNICEF imetoa msaada wa kisaikolojia kwa wavulana na wasichana 13,000 nchini humo na watoto wengine zaidi ya laki moja wamepata matibabu dhidi ya utapiamlo. 

Katika kupambana na malaria shirika hilo limeshagawa wajawazito na watoto vyandarua 148,000 vya ya kujikinga na mbu.

Na kupambana na maambukizi ya COVID-19 UNICEF imehakikisha watu wengine 260,000 wamepata huduma ya maji safi na salama.  

Shirika hilo limeahidi kuendelea kufanya kila juhududi kuhakikisha maisha ya mamilioni ya watoto wa Sudan Kusini yanaokolewa.