Pole Lebanon kwa tukio la leo, tuko pamoja katika hili- UN
Pole Lebanon kwa tukio la leo, tuko pamoja katika hili- UN
Kufuatia milipuko ya kutisha iliyotokea leo kwenye mji mkuu wa Lebanon, Beirut, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres, na Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa mataifa kwa wametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha kwenye matukio hayo huku akiwatakia ahueni ya harak majeruhi.
Taarifa iliyotolewa leo jijini New York, Marekani na Naibu msemaji wa Umoja wa Mataifa Farhan Haq, imesema kuwa miongoni mwa majeruhi ni wafanyakazi wa Umoja huo wanaofanya kazi nchini Lebanon.
Vyombo vya habari vimemnukuu Waziri wa Afya wa Lebanon akisema kuwa mlipuko huo mkubwa umesababisha vifo vya watu 70 na zaidi ya 2,700 wamejeruhiwa.
Katibu Mkuu amesema, “Umoja wa Mataifa umejizatiti kuendelea kusaidia Lebanon katika kipindi hiki kigumu na unashiriki kikamilifu katika kuchukua hatua kukabilia na tukio hili.”
Wakati huo huo Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Tijjani Muhammad-Bande ametuma salamu za rambirambi kwa familia zilizopoteza wapendwa wao katika mlipuko huo wa leo mjini Beirut huku akiwatakia majeruhi ahueni ya haraka.
Profesa Muhammad-Bande ameihakikishia Lebanon mshikamano nayo wakati huu.
Due to the explosion that rocked #Beirut Port today, one of our Maritime Task Force ships was damaged, leaving some naval peacekeepers injured. #UNIFIL is assessing the situation & stands ready to provide assistance & support to the Lebanese Government.ℹ️ https://t.co/8msy8IHJ3n
UNIFIL_
Walinda amani UNIFIL
Katika hatua nyingine, ujumbe wa muda wa Umoja wa Mataifa nchini Lebanon, UNIFL umethibitisha kuwa walinda amani kadhaa wamejeruhiwa.
Kwa mujibu wa taarifa ya UNIFIL, mlipuko huo umesababisha majeraha makubwa kwa wafanyakazi wanane wa kikosi kazi cha majini, MTF, na majeruhi kidogo kwa wengine kadhaa.
Majeruhi wote hao ni walinda amani kutoka Bangladesh na walikuwa katika jukumu ndani ya meli iliyokuwa imetia nanga bandarini Beirut.
Umoja wa Mataifa umeshauri wafnayakazi wake wasalie nyumbani huku Waziri Mkuu wa Lebanon Hassan Diab akitangaza kuwa kesho Jumatano ni siku ya maombolezo ya kitaifa.