Janga la COVID-19 linatupa fursa ya kuibadilisha miji yetu-Guterres

Janga la COVID-19 linatupa fursa ya kuibadilisha miji yetu-Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, kupitia ujumbe wake wa uzinduzi wa tamko la kisera kuhusu janga la virusi vya corona katika miji, hii leo ametoa wito kwa viongozi kote duniani kufikiria upya na kurekebisha miji katika kipindi hiki ambacho dunia inapona kutokana na janga la COVID-19 kwani miji imeonekana kuwa kitovu cha janga hilo.
Bwana Guterres ameeleza kuwa miji ni kitovu cha COVID-19 kwa kuwa asilimia ya wagonjwa wote wa janga hili wamethibitika kuwa wa mijini.
Katibu Mkuu Guterres amesema miji imejaa shida, mingi ikiwa na mifumo ya afya iliyoelemewa, huduma duni za maji na kujisafi pamoja na changamoto nyingine,“hii iko hususani katika maeneo maskini ambapo hali hii imefunua ukosefu wa usawa uliokita mizizi.”
Pamoja na hayo, Bwana Guterres ameeleza kuwa kwa upande mwingine, miji pia ni maeneo ambayo yameonesha mshikamano wa ajabu na ushujaa akisema kuwa dunia imeshuhudia, “watu wasiofahamiana wakisaidiana, mitaa ikiwashangilia kwa kuwaunga mkono wafanyakazi muhimu, wafanyabiashara wakitoa misaada ya kuokoa maisha.”
Katibu Mkuu Guterres pia amesema tunapopambana na janga hili la COVID-19 na kuelekea katika kupona, miji inapaswa kuangaliwa kama kitovu cha jamii, uvumbuzi wa mwanadamu na ustadi.
Bwana Guterres ametoa mapendekezo matatu likiwemo mosi kuhakikisha awamu zote za mapambano dhidi ya COVID-19 yanapambana pia na kukosekana kwa usawa katika jamii kwa kuwapa kipaumbele wle walioko hatarini ikiwemo kuwahakikishia malazi, pili kuimarisha uwezo wa serikali za mitaa na tatu kutafuta uchumi wa kijani, imara na jumuishi.