Ni miaka 25 ya kumbukumbu na kupata haki Srebrenica:Bachelet
Ni miaka 25 ya kumbukumbu na kupata haki Srebrenica:Bachelet
Leo ni miaka 25 tangu kufanyika mauaji ya kibari yaliyighubikwa na ukatili mkubwa zaidi duniani huko Srebrenica Bosnia na Herzegovina.
Katika ujumbe wake kuhusu siku hii Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet amesema “Mwaka huu tunaadhimisha kumbukumbu ya miaka 25 ya zahma kubwa ya kibinadamu na pia miaka 25 ya safari ndefu ya kupata kutambuliwa, haki na fidia kwa waathirika wa mauaji ya kimbari ya Srebrenica na uhalifu mwingine dhidi ya ubinadamu unaotambuliwa na mahakama za kimataifa.”
Ameongeza kwamba kumbukumbu hii inasisitiza umuhimu wa amani Bosnia Herzegovina na kuikumbusha dunia hali tete ya eneo hilo.
Amesema waandaaji wakuu wa moja ya unyama mbaya zaidi duniani wamekabiliwa na mkono wa sharia na mchakato unaendelea.”Lakini bado kuna kibarua kikubwa cha kufanya kuhakikisha uwajibikaji, kutenda haki kwa waathirika na kuchagiza uponyaji na maridhiano. Umoja wa Mataifa na nchi wanachama wana jukumu muhimu kuhakikisha kwamba viwango vya kimataifa vya haki za binadamu vinadumishwa.”
Kwa upande wa Bosnia Herzegovina Bi. Bachelet amewakumbusha kwamba changamoto bado zipo, makovu hayapona na kumbukumbu bado zinaumiza ila “Mtazamo mpya wa kitaifa unahitajika ili kusonga mbele mtazamo unaozingatia huruma, kuheshimiana na kuwasaidia waathirika na manusura.” lakini pia haja ya kila mtu kukabili majukumu yake kwani kukabiliana na historia kunahitaji kushughulikia hali ya sasa na ndio njia pekee ya kujenga mustakabali bora.
Kamishina huyo mkuu wa haki za binadamu amesisitiza kwamba kukana mauaji ya kimbari, kuwatukuza wahalifu wa vita waliohukumiwa na mitazamo mingine ambayo nikana ukweli na historia ni mifumo ya kauli za chuki na lazima ichukuliwe hivyo na wanasheria.
“Watu wa Magharibi wa Balkan wameumia sana kutokana na migogoro iliyosababishwa na chuki kwa ajili ya faida za masuala ya kisiasa. Maridhiano lazima yasakwe haraka na kwa vitendokwani wote walioathirika, kuuawa au kupoteza wapendwa wao Srebrenica na kwenye mzozo wa Balkan wanastahili hilo.”