Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya COVID-19, Uganda yafungua mpaka kwa muda kuruhusu wakimbizi kutoka DRC

Anurith, mkimbizi kutoka DRC akisaka hifadhi Uganda.
VIDEO YA UNHCR
Anurith, mkimbizi kutoka DRC akisaka hifadhi Uganda.

Licha ya COVID-19, Uganda yafungua mpaka kwa muda kuruhusu wakimbizi kutoka DRC

Wahamiaji na Wakimbizi

Hatimaye Uganda imeruhusu raia wa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC waliokimbia mapigano nchini mwao wapatiwe hifadhi baada ya kushindwa kuingia nchini humo tangu mwezi Mei mwaka huu kutokana na janga la ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19.

Uganda imefunga mipaka yake ya nje na pia imepitisha hatua za kuepusha kuchangamana ndani ya taifa hilo ambalo hadi sasa limeripoti kuwa na wagonjwa 889 na hakuna hata mmoja aliyefariki dunia.

Ripoti za maelfu ya raia wa DRC kukwama katika mpaka wa nchi mbili hizo, zilifikia wabunge wa Uganda ambao waliridhia kufunguliwa kwa muda mpaka kati ya Uganda na DRC kwa misingi ya kibinadamu kwenye vituo vya mpakani vya Zombo ili wakimbzi waweze kuingia na kupata huduma muhimu za kuokoa maisha.

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR, linasema kuwa kitendo cha Uganda kufungua mpaka wake wakati huu wa janga la COVID-19, ni ishara ya mshikamano na kinaonesha jinsi ya udhibiti wa mipaka huku ikifungua maeneo ya hifadhi.

Hilary Obaloker Onek, ambaye ni Waziri wa masuala ya misaada, majanga na wakimbizi amesema kuwa “hatujachoka, na hatuna ardhi ya kutosha, nchi yetu ni ndogo lakini bado tunawaruhusu kwa sababu ya huruma. Natamani jamii ya kimataifa nayo ingalikuwa na huruma na kusaidia watu hawa. Haya si matatizo yetu, haya ni matatizo ya dunia, matatizo ya kimataifa.”

Kwa sasa UNHCR inashirikiana na serikali ya Uganda na wadau wake kupatia wakimbizi hao misaada na huduma muhimu ikiwemo chakula na malazi huku ikishirikiana na Wizara ya afya kuhakikisha kuwa wakimbizi wanapimwa iwapo wana virusi vya Corona au la, na hatua sahihi zichukuliwe.

Akifafanua zaidi Philippy Creppy, ambaye ni Mwakilishi msaidizi wa UNHCR nchini Uganda akihusika na operesheni amesema kuwa“bila shaka tunaweka malazi, upimaji wa COVID-19. Kama unavyofahamu, hii ni dharura ya kipekee. Ni mara ya kwanza watu wanavuka mpaka katikati ya janga la Corona. Lazima tuwe makini tuweke mambo yote pamoja, uchunguzi wa kiusalama, COVID-19 na Ebola. Kama ujuavyo bado Ebola ipo DRC. Timu yetu inachukua kila hatua kuwa tayari.”

Baada ya uchunguzi wa awali, wasaka hifadhi wanasafirishwa na UNHCR hadi kituo cha karantini kilichoko kilometa 13 kutoka mpakani ambapo baada ya siku 14 za karantini ya lazima, watahamishiwa katika makazi yaliyopo ya wakimbizi.

Nchini Uganda, wakimbizi na wasaka hifadhi wanajumuishwa katika mipango na shughuli za kitaifa za usimamizi, maandalizi na utekelezaji.