Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Heko Somalia kwa upimaji wa COVID-19:UN 

Wahudumu wa afya katika kiliniki inayosaidiwa na UN karibu na kambi ya wakimbizi wa ndani ya Ceel Jaale katika eneo la Belet Weyne wakimuhudumia mama na bintiye mdogo.
UNSOM
Wahudumu wa afya katika kiliniki inayosaidiwa na UN karibu na kambi ya wakimbizi wa ndani ya Ceel Jaale katika eneo la Belet Weyne wakimuhudumia mama na bintiye mdogo.

Heko Somalia kwa upimaji wa COVID-19:UN 

Afya

Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia James Swan ameipongeza serikali ya Somalia kwa juhudi kubwa inazozifanya katika upimaji wa virusi vya corona au COVID-19 baada ya leo kuzuru maabara ya taifa ya afya ya umma (NPHRL) mjini Moghadishu.

 

Bwana Swan amekaribisha pia hatua za kuwajengea uwezo wahudumu wa afya kwa ajili ya siku za usoni amesema “Katika miezi minne iliyopita maabara ya kitaifa imekuwa na jukumu kubwa na muhimu katika hatua za kupambana na mlipuko wa COVID-19 kwa kubaini wagonjwa na kufuatilia mzunguko wa virusi. Maabara hiyo kuu imekuwa ikishirikiana na maabara zingine mbili za umma kwa ajili ya upimaji wa COVID-19, na hii imeisaidia Somalia kupima na kufuatilia mzunguko wa maambukizi nchi zima na kubaini maeneo yenye maambukizi makubwa kwa ajili ya kuyadhibiti mapema.”

Mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, James Swan akihutubia Baraza la Usalama.
UN Photo/Manuel Elías
Mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, James Swan akihutubia Baraza la Usalama.

Bwana Swan ambaye pia ni mkuu wa mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia UNSOM, amesisitiza kwamba “Upimaji wa virusi vya COVID-19 ni muhimu na Umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa wamedhamiria kuisaidia maabara hiyo ya kitaifa."

Ameongeza kuwa hatua kubwa za uwezo wa Somalia kupambana na COVID-19 zinaonyesha ni nini kinachoweza kufikiwa endapo taifa na wataalam wa kimataifa watafanyakazi bega kwa bega.”

Katika ziara ya leo  bwana. Swan aliambatana na mwakilishi wa shirika la afya duniani WHO nchini Somalia Dkt. Mamunur Rahman Malik. 

 

Baada ya mlipuko wa Corona nchini Somalia WHO iliipatia maabara hiyo msaada wa machine za kupima corona na kuiwezesha kuwapima watu wengi na kuokoa maisha ya maelfu ya watu. Kwa sasa mashine hizo zina uwezo wa kupima wagonjwa 180 kwa siku.

Na hadi kufikia leo karibu watu 7,000 wameshapimwa  na zoezi linaendelea licha ya kuwepo kwa changamoto zingine kama vita.

Umoja wa Mataifa unaziona maabara hizo kama ni uwekezaji mkubwa kwa ajili ya mustakabali wa Somalia na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa yamechangia kwa kiasi kukubwa kufanikisha hilo,  likiwemo shirika la mpango wa chakula duniani WFP, la maendeleo UNDP na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya msaada kwa Somalia UNSOS.