Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tuunge mkono biashara ndogo na za kati wakati huu wa COVID-19- UN

Fundi cherehani raia wa Jamhuri wa Kidemokrasi ya Congo- DRC lakini akiishi kama mkimbizi Kenya.
© UNHCR/Rose Ogola
Fundi cherehani raia wa Jamhuri wa Kidemokrasi ya Congo- DRC lakini akiishi kama mkimbizi Kenya.

Tuunge mkono biashara ndogo na za kati wakati huu wa COVID-19- UN

Ukuaji wa Kiuchumi

Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya biashara ndogo na za kati, SMEs, Umoja wa Mataifa unataka hatua zaidi zichukuliwa kusaidia sekta hii kwa kuwa imeathirika zaidi wakati huu wa janga la ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19.
 

Kupitia wavuti wa siku hii, Umoja wa Mataifa unasema kuwa, biashara ndogo na za kati ikiwemo zile zinazoendeshwa na wanawake na vijana wajasiriamali zimetikishwa na anguko la kiuchumi litokanalo na COVID-19

“Hatua zisizo za kutarajiwa za kuzuia kuchangamana na kuwekwa karantini kwa lengo la kuzuia kuenea kwa virusi vya Corona, zimevuruga mnyororo wa usambazaji wa bidhaa na kusababisha anguko kubwa la mahitaij ya bidhaa katika sekta nyingie,”  umesema Umoja wa Mataifa.

Ili sekta hizo ziweze kuendelea na dhima yake muhimu ya kuweka mazingira ya ajira zenye utu huku zikiboresha maisha ya watu, “biashara ndogo kwa kiasi kikubwa zinategemea mazingira wezeshi, ikiwemo msaada wa kupata fedha, taarifa na masoko.

Umoja wa Mataifa unasema kuwa “hebu tusisahau kuwa biashara hizi, ambazo kwa kawaida huajiri watu wasiozidi 250, ndio uti wa mgongo wa chumi nyingi duniani na zina nafasi muhimu katika nchi zinazoendelea.” 

Kwa mujibu wa takwimu za Baraza la kimataifa la biashara ndogo ndogo duniani, ICSB, biashara ndogo na za kat izilizo na zisizo rasmi ni asilimia 90 ya kampuni na kwa wastani hutoa asilimia 70 ya ajira na asilimia 50 ya pato la ndani la nchi, GDP.

Ni kwa kutambua umuhimu wa biashara hizo ndio maana Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitangaza kuwa tarehe 27 mwezi juni iwe siku ya kutambua mchango wa kampun ihizo katika maendeleo endelevu na uchumi wa dunia.
Kwa upande wake, kituo cha biashara cha kimataifa, ITC, ambacho ni shiirika tanzu la kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa, UNCTAD, kinafuatilia jinsi janga la COVID-19 limeathiri kampuni ndogo na za kati ikijikita zaidi kwa biashara ndogo kwenye nchi zinazoendelea.

ITC inapigia chepuo uboreshaji wa mazingira ya biashara katika kampuni hizo ambapo moja ya kampuni iliyonufaika na ushauri huo ni  ile ya Trianon ambayo inahusika na kupata bidhaa za viungo kutoka kwa wakulima na kuziuza nje ya nchi.

Trianon ni ubia kati ya kampuni ya Uholanzi ya mtaalamu wa viungo, Paul de Rooji, Bapa na ya kitanzania Companero Farmers. na sasa inasafirisha viungo kwenda Ulaya.

Trianon pamoja na kuchukua hatua za mazingira pia imewekeza katika afya ya jamii ambako inapata mazao yake na imetumia dola 5,000 kutokana na mauzo yake ya kwanza kununua aproni 100,000, barakoa 200 za kufua na kutumia tena na barakoa 2,000 za kitabibu kwa ajili ya hospitali.

Licha ya mlipuko wa COVID-19, Trianon iliweza kukamisha oda zake na kusafirisha shehena kwenda Rotterdam na Italia.