Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkimbizi atumia stadi za uchungaji kunusuru watu na COVID-19

Mkimbizi Djuba Dionis kutoka DRC akitumia stadi zake za uhubiri kuelimisha wenzake kambini Kakuma nchini Kenya kuhusu jinsi ya kujikinga na COVID-19.
UNHCR Video
Mkimbizi Djuba Dionis kutoka DRC akitumia stadi zake za uhubiri kuelimisha wenzake kambini Kakuma nchini Kenya kuhusu jinsi ya kujikinga na COVID-19.

Mkimbizi atumia stadi za uchungaji kunusuru watu na COVID-19

Wahamiaji na Wakimbizi

Nchini Kenya katika kambi ya wakimbizi ya Kakuma, Djuba Alois mkimbizi mwenye umri wa miaka 75 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, anatumia kipawa chake cha uhubiri kuelimisha watu kuhusu ugonjwa wa virusi vya Corona, COVID-19 na jinsi ya kujikinga.

Bwana Alois, katika video ya shirika la kuhudumiwa wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR, anasema kuwa, aliposikia kuhusu janga la kidunia kuhusu COVID-19“nilichanganyikiwa kutokana na idadi ya waliokuwa wameambukizwa na kufariki dunia kutokana na ugonjwa huo duniani kote.”

Ni kwa mantiki hiyo Bwana Alois aliamua kutumia kipaji chake cha uchunguaji kuelimisha watu kuhusu jinisi ya kujilinda na COVID-19 kambini.

Mkimbizi huyu alianza kutengeneza mabango ya matangazo na kuyaweka kwenye baiskeli yake baada ya kuona kwenye simu ya Rafiki yake jinsi watu wanafariki dunia barani Ulaya.

Hivi sasa UNHCR na wadau na wakimbizi wenyewe wanafanya kazi kuhakikisha kuwa taarifa kuhusu gonjwa hilo ni sahihi na zinasambazwa kwa watu wote.

Bwana Alois anasema,“kuwa makini,virusi vinaua. Niliona kwenye simu ya Rafiki yangu jinsi watu wanakufa huko Ulaya, moyo wangu ulizizima.

Na sasa anatoa wito akisema kuwa, “tafadhali nawa mikono yako, na usiponawa utajuta. Sasa nitaelimisha watu kila siku ili watu wajikinge na virusi. Rafiki zangu, wapendwa wangu,  nataka kuwasaidia.”