Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Pamoja na kulinda amani, TANZBATT 7 yatoa msaada hospitali kuu Beni

Kikosi cha 7 cha Tanzania kwenye ujumbe wa UN nchini DRC, MONUSCO wakikabidhi msaada wa dawa kwa hospitali kuu ya Beni jimboni Kivu Kaskazini.
TANZBATT 7 Video
Kikosi cha 7 cha Tanzania kwenye ujumbe wa UN nchini DRC, MONUSCO wakikabidhi msaada wa dawa kwa hospitali kuu ya Beni jimboni Kivu Kaskazini.

Pamoja na kulinda amani, TANZBATT 7 yatoa msaada hospitali kuu Beni

Amani na Usalama

Hospitali kuu ya Beni jimboni Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC imeshukuru msaada wa dawa kutoka kikosi cha Tanzania kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini  humo, MONUSCO  ikisema kuwa msaada huo umekuja wakati muafaka. 

Msaada huo wa dawa umewasilishwa katika hospitali kuu ya dayosisi ya Butembo mjini Beni jimbo la Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na walinda amani kutoka kikosi cha 7 cha Tanzania, TANZBATT 7,  kwenye kikosi cha kujibu mashambulizi, FIB,  cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO.

Dkt. Frank Muhindo Fikiri ni Mkurugenzi wa hospitali hiyo na amesema kuwa, "eneo hili linakabiliwa sana na mashambulizi,  wakimbizi,  watoto wachanga wasio na chakula, wazazi  wanaojifungua bila msaada wowote.Tunafurahi na tunaona huo msaada utasaidia kuongeza uwezo wetu wa kuwahudumia wagonjwa mbalimbali wanaopatikana hapa hospitali. Na isiwe dawa tu hata chakula. Tunashukuru sana ndugu zetu hawa kutoka Tanzania."

Kwa upande wake, Dkt Joseph Mkandara kutoka TANZBATT 7, anafafanua kuhusu msaada wao akisema kuwa, "tumetoa kiasi cha dawa kutoka zile ambazo tungetumia  na tukaona  dawa kiasi wasaidie wagonjwa waliopo hapa hospitali ya Beni ,ni dawa kidogo lakini tuna imani kwamba zitawasaidia."

Private Jeniffer Mbogo ni mlinda amani kutoka Tanzania anasema na anasema kuwa,  "tumekuja hapa hospitali ya Beni ili kuleta dawa kama msaada ili kuwasaidia akina mama pamoja na watoto.. Unajua katika vita, wanaopata shida zaidi ni akina mama na watoto"