Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtaa kwa mtaa, nyumba kwa nyumba hadi COVID-19 ilieleweke- UNMISS

Walimu wamekuwa wakifanyakazi ya kuelimisha wanajamii kuhusu COVID-19 katika mipango ya elimu iliyotangazwa kwenye Radio Miraya, ambayo inaendeshwa na ujumbe wa kulinda amani wa UN huko Sudan Kusini
UNMISS
Walimu wamekuwa wakifanyakazi ya kuelimisha wanajamii kuhusu COVID-19 katika mipango ya elimu iliyotangazwa kwenye Radio Miraya, ambayo inaendeshwa na ujumbe wa kulinda amani wa UN huko Sudan Kusini

Mtaa kwa mtaa, nyumba kwa nyumba hadi COVID-19 ilieleweke- UNMISS

Afya

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS, umezindua kampeni ya siku tano ya kuelimisha umma kuhusu ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19 kwenye maeneo manne yenye wakazi wengi zaidi eneo la Equatoria Magharibi.

Ujumbe wa kuelimisha watu kuhusu COVID-19 ukisikika kutoka kwenye Pikipiki ya magurudumu matatu hii iliyofungwa spika kubwa, ikipita mtaa kwa mtaa kwenye mji wa Yambio, jimboni Gbudue ukanda wa Equatoria Magharibi nchini Sudan Kusini, kulikoni? Tahiru Ibrahim, ni Kaimu Mkuu wa ofisi ya UNMISS huko Yambio jimboni Gbudwe na anasema wamechukua hatua hiyo kuunga mkono juhudi za serikali ya Sudan Kusini kwa kuwa,.

“Baadhi ya watu hawataki kuamini kuwa hii COVID-19 ni kitu cha ukweli. Lakini tunahitaji kuendelea na juhudi za kuwaelimisha wananchi ili waweze kukubali ukweli kwamba ugonjwa huu upo na tunahitaji kuzingatia kanuni ili tuweze kuwa salama.”

Hadi sasa Sudan Kusini ina wagonjwa zaidi ya 1,600 na kati yao hao 20 wamefariki dunia, katika taifa hilo ambalo kutokana na mazingira yake, kutochangamana bado ni tatizo kubwa.

Vipeperushi vinavyosambazwa sambamba na ujumbe utolewao kwenye spika hizo vimezingatia mwongozo wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO.

Wilson Thomas Yanga,  ni mkuu wa kikosi kazi cha kukabiliana na COVID-19  huko Gbudue ambako tayari kuna mgonjwa wa Corona. Pamoja na kutaka raia wa Sudan Kusini watambue hatari za ugonjwa huo anasema..

“Ni wajibu wa wa kila mtu kufahamisha watu ya kwamba virusi vya Corona ni vya ukweli na vipo. Hasa hapa Yambio ambako tuna wagonjwa. Ijapokuwa watu wengi wamepita nyumba kwa nyumba kuelimisha kuhusu hatari za virusi vya Corona, nielewavyo mimi watu bado hawazingatii kanuni za kujikinga. Kwa hiyo tunahitaji kuongeza bidii kuhakikisha taarifa zinafikia wale wa vijijini na kila mahali ili watu wajue kuwa ugonjwa huu hatari hauna tiba wala chanjo. Chanjo na tiba pekee ni kujikinga.”

Mkuu huyo wa kikosi kazi cha kupambana na COVID-19 Gbudue, ameshukuru wadau hususan UNMISS ambao amesema wako nao nyakati za amani na vita na katika janga la sasa.

UNMISS inasema kuwa kwa jamii nchini Sudan Kusini, bado suala la kutochangamana ni changamoto kubwa.