Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bi. Mrema kutoka Tanzania kuongoza sekretarieti ya Bayonuai ya kibailojia

Elizabeth Maruma Mrema kutoka Tanzania ameteuliwa na Katibu Mkuu wa UN kuwa Katibu Mtendaji wa Sekretarieti ya Mkataba wa Kimatafa wa Bayonuai ya kibaiolojia, CBD.
UNEP
Elizabeth Maruma Mrema kutoka Tanzania ameteuliwa na Katibu Mkuu wa UN kuwa Katibu Mtendaji wa Sekretarieti ya Mkataba wa Kimatafa wa Bayonuai ya kibaiolojia, CBD.

Bi. Mrema kutoka Tanzania kuongoza sekretarieti ya Bayonuai ya kibailojia

Masuala ya UM

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amemteua Elizabeth Maruma Mrema kutoka Tanzania kuwa Katibu Mtendaji wa Sekretarieti ya Mkataba wa Kimatafa wa Bayonuai ya kibaiolojia, CBD.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Stéphane Dujarric akizungumza na waandishi wa habari jijini New York, leo kwa njia ya video amesema kuwa, tangu mwezi Desemba mwaka 2019 Bi. Mrema amekuwa akikaimu wadhifa huo na sasa ameteuliwa rasmi.

Kabla ya kujiunga na sekretarieti hiyo yenye jukumu la kusimamia utekelezaji wa mkataba wa kimataifa wa bayonuai ya kibaiolojia, Bi. Mrema alikuwa Mkurugenzi wa Idara ya Sheria ya shirika la mazingira la Umoja wa Mataifa, UNEP jijini Nairobi, Kenya.

Mkataba wa kimataifa wa bayonuai ya kibaiolojia, ulitiwa saini huko Rio de Janeiro, Brazil, mwaka 1992 na kuanza rasmi kutumika tarehe 29 mwezi Desemba mwaka 1993.
Mkataba huu ni wa kwanza wa kimataifa ukijumuisha aina zote za bayonuai ya kibaiolojia: uhifadhi wa bayonuai ya kibaiolojia, matumizi yake endelevu na mgao sawa wa manufaa yake yatokanayo na rasilimali za kijenetiki.
Bayonuai ya kibaiolojia hujumuisha viumbe hai vikiwemo vya ardhini na majini.

Wanyama kama huyu simba marara wako hatarini kutoweka na hivyo kuharibu bayonuai ya kibaiolojia.
UN /John Isaac
Wanyama kama huyu simba marara wako hatarini kutoweka na hivyo kuharibu bayonuai ya kibaiolojia.

Akiwa na uzoefu wa zaidi ya miongo miwili kwenye Umoja wa Mataifa, Bi. Mrema anashika wadhifa huo wa Katibu Mtendaji akiwa na ubobezi kwenye sheria za kimataifa za mazingira na utungaji sera pamoja na utekelezaji wa miradi ya kimataifa ya mazingira na maendeleo endelevu.

Tangu mwaka 2009 hadi 2012, ameshika nyadhifa kadha ikiwemo Katibu Mtendaji wa UNEP kwenye sekretarieti ya Mkataba wa Kimataifa wa uhifadhi wa viumbe pori vinavyohamahama .

Kabla ya kujiunga na UNEP, Bi. Mrema amefanya kazi kwenye Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa nchini Tanzania ambapo pia wakati huo alikuwa akifundisha chuo cha Diplomasia.

Bi. Mrema ana shahada ya Uzamili kwenye sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dalhousie, Halifax, nchini Canada, Stashahada ya Uhusiano wa Kimataifa na Diplomasia kutoka Chuo cha Diplomasia Dar-es-Salaam, Tanzania, na shahada ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nchini Tanzania.