Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Pika chakula hadi kiive na tenganisha kibichi na kilichoiva - WHO

Nyama ikiwa katika soko la Hamarwayne, Mogadishu Somalia.
AMISOM/Omar Abdisalan
Nyama ikiwa katika soko la Hamarwayne, Mogadishu Somalia.

Pika chakula hadi kiive na tenganisha kibichi na kilichoiva - WHO

Afya

Leo ni siku ya kimataifa ya usalama wa chakula ikilenga kuangazia na kuhamasisha juhudi za kuzuia, kubaini na kudhibiti hatari zitokanazo na ulaji wa vyakula katika hali inayoweza kusababisha magonjwa.

Shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO, linasema kuwa chakula salama kinasaidia uwepo wa uhakika wa chakula, afya ya binadamu, ustawi wa kiuchumi, kilimo, masoko, utalii na maendeleo endelevu

Mwaka huu maadhimisho ya siku hii yanaimarisha wito uliotolewa mjini Addis Ababa, Ethiopia na Geneva Uswisi kuhusu mustakbali wa usalama wa chakula ujumbe ukiwa usalama wa chakula ni jukumu la kila mtu.

WHO kupitia wavuti wake inasema kuwa usalama wa chakula ni wajibu wa pamoja baina ya serikali, wazalishaji na walaji, “kila mtu ana jukumu lake kuanzia shambani hadi mezani, kuhakikisha kuwa chakula tunachokula ni salama na hakitakuwa na madhara ya kiafya,” imesema WHO.

Mke wa Bwana Sawadogo akiandaa chakula baada ya kupata mgao kutoka WFP huko Kaya, nchini Burkina Faso.
WFP/Mahamady Ouedraogo
Mke wa Bwana Sawadogo akiandaa chakula baada ya kupata mgao kutoka WFP huko Kaya, nchini Burkina Faso.

Kupitia maadhimisho haya, WHO inasaka juhudi za kujumuisha suala la usalama wa chakula kwenye ajenda ya umma na kupunguza mzigo utokanao na magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya chakula duniani kote.

Akizungumzia maadhimisho haya ambayo ni ya pili tangu Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lipitishe azimio kuhusu siku hii, Dkt. Francesco Branca, ambaye ni mkuu wa Idara ya Lishe na Usalama wa Chakula, WHO, amesema kuwa, “usalama wa chakula ni suala la umma. Je unafahamu kuwa kila mwaka, mtu mmoja kati ya watu 10, anaugua baada ya kula chakula chenye sumu na watu 420, 000 wanafariki dunia wakiwemo watoto 125,000 wenye umri wa chini ya miaka 5 .”

Ni kwa mantiki hiyo anasema “kuwa katika siku hii tunataka kuhamasisha kila mtu asaidie kupunguza hatari za magonjwa yatokanayo na ulaji wa chakula kisicho salama, wale wanaozalisha, wanaosafirisha, wanaouza, wanaoandaa na kusambaza chakula na wale wanaokula. “

Dkt. Branca anasema kuwa hakikisha pale unapoandalia chakula ni pasafi, tenganisha chakula kibichi na kile kilichopikwa, pika chakula hadi kiive, hifadhi chakula katika joto linalotakiwa, tumia maji na viambato vilivyo safi na salama.

Wahamiaji wakiandaa samaki kwa ajili ya mauzo katika soko moja mjini Dubai
ILO/Deloche P
Wahamiaji wakiandaa samaki kwa ajili ya mauzo katika soko moja mjini Dubai