Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika yaweza kujijenga upya baada ya COVID-19

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi Amina Mohamed akihutubia kikao cha ufunguzi cha mkutano wa sehemu ya mawaziri cha jukwaa maalum kuhusu maendeleo endelevu SDGs
UN Photo/Loey Felipe
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi Amina Mohamed akihutubia kikao cha ufunguzi cha mkutano wa sehemu ya mawaziri cha jukwaa maalum kuhusu maendeleo endelevu SDGs

Afrika yaweza kujijenga upya baada ya COVID-19

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Huu ni wakati mgumu kwa Afrika na ulimwengu wetu wote ulio kama  kijiji.Kufikia tarehe 24 Mei 2020, mataifa 54 katika bara Afrika yalikuwa yamerekodi zaidi ya wagonjwa 100,000 wa COVID-19 na zaidi ya vifo 3,000. Na huku idadi ya wagonjwa  ikiendelea kuongezeka, hali ingekuwa mbaya zaidi kama serikali za Afrika hazingechukua hatua za kuzuia licha ya mazingira dhaifu.

Tunaomboleza vifo waliofariki na kutambua majonzi na mzigo wa jamaa na wapendwa waliowachwa nyuma. Maisha kama tulivyoyajua, yamebadilika kwa njia zisizokadirika. Chumi na vitegauchumi vimeathirika sana huku utashi wa bidhaa za Afrika ukishuka na utalii kuanguka mno. Pesa zinazotumwa nyumbani kutoka ughaibuni ambazo zinaweza kuwa zaidi ya asilimia 10 ya Pato la Kitaifa (GDP) zinadidimia.

Tayari bei ya mafuta, ambayo ni asilimia 40 ya mauzo ya Afrika nje na asilimia 7.4 ya Pato la Kitaifa yamepungua kwa nusu, na kuathiri kwa kiasi kikubwa mapato ya mataifa kama Nigeria na Angola. Kuanguka huko kwa bei kama ya kahawa na kakao kumepunguza mapato kwa mataifa ya Uhabeshi, Kenya, Côte d'Ivoire na mengine yanayozalisha bidhaa hizi.

Wafanyikazi wa sekta zisizo rasmi, ambao ni asilimia 85.8 ya wafanyakazi, wasio na ulinzi wa wa kijamii na vizuizi dhidi ya mawimbi ya kiuchumi, wanakabiliwa na athari mbaya. Hili haswa linawahusu wafanyakazi wa kike ambao ni sehemu kuu ya sekta hiyo.

Ukuaji wa uchumi wa Afrika waweza kupungua kwa asilimia 2.6, na kudidimiza takribani watu milioni 29 zaidi katika lindi la umaskini. Huku idadi ikiongezeka, masomo yamesitishwa, na kuwatoa wanafunzi shuleni, na kuzua taharuki kuhusu iwapo wataendelea na masomo yao na wakati uo huo kupoteza ufanisi ambao umepatikana kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Naibu Katibu Mkuu wa UN Amina J. Mohammed akihutubia mkutano wa Umoja wa Mataifakutoka maktaba Oktoba 22, 2018
IISD/ENB
Naibu Katibu Mkuu wa UN Amina J. Mohammed akihutubia mkutano wa Umoja wa Mataifakutoka maktaba Oktoba 22, 2018

Uhaba wa chakula, ikiwa ni pamoja na mahindi, mafuta ya kupika na unga wa ngano, unaweza kusababisha hatari ya ukosefu wa chakula iwapo matatizo kama mawingu ya nzige wanaoharibu mimea na nyasi za mifugo katika eneo la Afrika Mashariki hayatakabiliwa. Uvurugaji wa mikondo ya ugavi wa kimataifa pia unaathiri sana uwezo wa kuuza nje ya Afrika.

Janga hili pia limeweka wazi udhaifu wa muda mrefu na ukosefu wa usawa, ikiwa ni pamoja na tatizo sugu la ubaguzi wa wanawake na wasichana.  Kumekuwa pia na ongezeko la kutisha la viwango vya dhuluma nyumbani, na ukiukaji wa haki katika kipindi cha amri ya kusalia nyumbani. Hizi ni baadhi ya ripoti tuzipatazo kila siku, visa vya uchungu, wasiwasi, kukata tamaa na maumivu makali. Lakini kuna matumaini pia, yaliyojikita katika moyo wa kitamaduni wa mshikamano, utu, wa Ubuntu “ nipo kwa kuwa tupo.”

Madaktari, wauguzi, wahudumu wengine wa afya na wananchi wa kawaida, wanaume na wanawake, wazee kwa wachanga, wanadhihirisha kujitolea, ujasiri na udhati wa nafsi dhidi ya janga hili. Wanawake ni zaidi ya asilimia 70 ya wahudumu wa afya; wanahatarisha maisha yao kuwaokoa wengine, wakihudumu kama wauguzi, dobi, wapishi wasaidizi miongoni mwa wengine.

Uongozi wa Umoja wa Afrika (AU) uliwajibikia hatari hii haraka, ukiweka mwelekeo wa ushirikino wa bara zima, ukaweka Mpango wa Kifedha wa Kukabili COVID-19 na kuwateua wajumbe maalumu kuandaa msaada wa kimataifa. Umoja wa Mataifa, ukiongozwa na Shirika la Chakula Duniani (WHO) na Dr. Tedros Ghebreyesus, limejiandaa kuzisaidia serikali za Afrika kujitayarisha kwa, kuwajibika na kukomesha janga hili. Kituo Cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Amoja wa Afrika (Africa CDC) kinashirikiana na WHO na washirika wengine kutoa mafunzo na mahitaji ya matibabu kwa mataifa.Vijana wa Afrika wanajitokeza na masuluhisho ya kiubunifu kukabili changamoto za huduma za kiafya. Nchini Cameroon, kwa mfano, Christian Achaleke, wa miaka 26 aliwaunganisha marafiki na wafanyakazi wenzake kuzindua kampeni ya “Mtu mmoja Kieuzi Kimoja.” Aliwekeza mshahara wake kuanzisha uzalishaji wa vieuzi nyumbani kwa kutumia mwongozo wa WHO.  

Serikali zimetangaza mipango ya misaada. Kampuni zinabadilisha uzalishaji wake kuunda barakoa, vieuzi, majoho miongoni mwa bidhaa nyinginezo.Zaidi ya uwajibikaji wa kiafya, Shirika la Umoja wa Mataifa liliimarisha upesi shughuli zake za amani na usalama, mfululizo wa masuala ya kibinadamu na maendeleo ili kusaidia uwajibikaji wa Afrika kuhusu COVID-19. Umoja wa Afrika umezindua Mpango wa Kimataifa wa kibinadamu, ambao mgao wake mkuu unalenga bara Afrika. "Solidarity Flights" za Umoja wa Mataifa na Shirika la Chakula Duniani (WFP) kwa ushirikiano na AU na Africa CDC, wanawasilisha vifaa vya matibabu vinavyohitajika kwa dharura kwa mataifa yote ya Afrika.

 

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed akimtazama mwanafunzi wa shule ya msingi Ruiru wakati akila mlo  unaopatikana kupitia apu ya Tap2Eat
UNEP/Jane Smith
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed akimtazama mwanafunzi wa shule ya msingi Ruiru wakati akila mlo unaopatikana kupitia apu ya Tap2Eat

Timu za Umoja wa Mataifa pamoja na balozi zake katika mataifa zinatoa huduma jumuishi kwa kutumikisha uwezo wa wa mashirika mmahususi, fedha na mipango. Huku ukiongozwa na  Taratibu Wajibika za Kiuchumi na Kijamii, Umoja wa Mataifa anashirikiana na serikali za Afrika kushughulikia Athari za kiuchumi na kijamii za hatari hii, kuanzia kuhakikisha kuna huduma muhimu za kiafya, ulinzi wa kijamii na huduma msingi, kulinda ajira, kuongoza sera za hazina za serikali na mipango mikuu na kuwezesha mshikamano wa kijamii pamoja na ustahimilivu wa jamii. Kwa mfano, nchini Kenya, Nigeria, Afrika Kusini, na Zambia, Umoja wa Mataifa umeshirikiana na serikali na washirika wa kimaendeleo kuandaa raslimali za kifedha.

Nchini Burkina Faso, Gabon, Mali na Tunisia, Umoja wa Mataifa unazisaidia serikali katika harakati za kupata Vifaa vya Kujilinda (PPEs). Nchini Uhabeshi, Umoja wa Mataifa—kupitia WFP—unatoa msaada wa usafiri kusaidia uwasilishaji wa bidhaa kutoka kwa wadhamini wa kibinafsi. Mpango wa Umoja wa Mataifa  Multidimensional Integrated Stabilization Mission katika Central African Republic (MINUSCA) umefadhili vipindi vya habari za COVID-19 kwa watumishi wa umma na wahudumu wa kijamii na kugawa vifaa  vya habari vigawiwe wanajeshi na wanajamii kwa jumla.  

Naibu Katibu Mkuu Amina Mohammed (Desemba 2019)
UN Video
Naibu Katibu Mkuu Amina Mohammed (Desemba 2019)

 

Na Shirika la Uimarishaji la Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (MONUSCO) linatumia kituo chake cha redio kuwafahamisha watu kuhusu COVID-19 kwa lugha asilia, ikijaribu kukabili uvumi na parojo.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameomba zaidi ya dola bilioni 200 zitolewa kwa Afrika kama sehemu ya mgao wa uwajibikaji mkamilifu wa kimataifa, pamoja na kusitisha ulipaji madeni kote, chaguzi kuhusu uendelezi wa madeni na masuluhisho kwa masuala ya taratibu za kimataifa kuhusu madeni.

Zaidi ya hayo, Umoja wa Mataifa, kwa ushirikiano na AU na Jumuiya ya Ulaya umetia sahihi mpango wa kikanda wa Spotlight kumaliza Dhuluma dhidi ya Wanawake na wasichana, huku ukilenga dola milioni 40 kwa juhudi za uzuiaji na uwajibikaji.Hizi habari njema zinaweka matumaini. Miezi michache iliyopita, hali ya Afrika ilikuwa ikiimarika. Baadhi ya chumi zinazokua kwa kasi ulimwenguni zilikuwa katika bara Afrika. Ukuaji wa intanenti ulipanua ubunifu kwa Wafrika, haswa vijana.

Kushuka kwa viwango vya umaskini na vifo vya watoto kuliashiria Afrika ilikuwa katika njia nzuri ya maendeleo, ikikitwa katika Ajenda ya Maendeleo Endelevu ya 2030 na Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika.Tunastahili kuamini kwamba hili ni janga dogo na kwamba Afrika itang’aa tena—kwa sababu ya vijana wa Afrika, ubunifu na ushirikiano wao  halisi kujikomboa vyema. Maingilianoya mataifa ya Afrika, haswa jamii za mipakani yahitaji kwamba bara hili liendelee kutegemea mshikamano wa Waafrika katika kukabili COVID-19. Methali ya kiafrika “Bila viganja viwili kofi hazilii” ina ukweli sasa kama kitambo.

 Kujikomboa vyema

Licha ya athari mbaya ya janga hili, Afrika inaweza kujenga upya vyema. Hapa kuna njia chache za kufanya hivyo:

Kwanza, imarisha kuwepo kwa bidhaa za kimatibabu kwa kuweka njia wazi katika ofisi za forodha kuwezesha usafirishaji haraka, kusimamisha ushuru wa forodha kwa bidhaa za kimatibabu, kuweka utaratibu wa kudhibiti bei na kuwezesha utengenezwaji wa bidhaa za kimatibabu hapa nchini.

Pili, kulinda biashara ndogo na zile wastani, ikiwa ni pamoja na kuinua nafasi katika uchumi wa kidijitali na kupanua upatikanaji wa teknolojia.

Tatu, tekeleza Soko Huru la Bara Afrika ili kuongeza kasi ya ukuaji wa viwanda vya Afrika na kuimarisha uchumi wake ili uweze kuhimili mawimbi ya kimataifa katika siku za usoni.  

Nne, tumia uokoaji kuongeza kasi ya kuanza kutumia kaboni ya kiwango kidogo, ukuaji usiotikiswa na mabadiliko ya tabianchi, na kuhamia katika chumi zinazojitenga na uchafuzi wa hewa, kubuni nafasi za ajira zisizochafua mazingira, na kuhakikisha matumizi pamoja na uzalishaji safi na endelevu. 

Tano, tunastahili kutilia maanani zaidi watoto, wazee, walemavu, wakimbizi wa kimataifa na wa ndani kwa ndani.  

Mwongozo wa taratibu zetu nzuri na endelevu za uokoaji ni Ajenda ya Maendeleo Endelevu na Makubaliano ya Paris kuhusu Tabianchi.  Ni lazima wamawake washiriki katika maamuzi. Ni lazima pia tutumie vipaji vya vijana kama tunataka kufaulu katika kuibadilisha Afrika kuwa bara la ushirikishi na maendeleo yatakayonufaisha vizazi vya siku za usoni. Tutalishinda janga hili pamoja. COVID-19 yaweza kushindwa barani Afrika, tunaweza kujenga upya pamoja. Kwa maneno ya Nelson Mandela: “Ni jukumu lako kujenga ulimwengu bora kwa wote wanaoishi ndani yake.”

 

Makala hii ilichapishwa mwanzo na   Afric Renewal, jarida la Umoja wa Mataifa.