Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu 1,300 wauawa DRC kwa kipindi cha miezi 8:OHCHR

Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet
UN Photo/Antoine Tardy
Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet

Watu 1,300 wauawa DRC kwa kipindi cha miezi 8:OHCHR

Haki za binadamu

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa leo imesema takribani watu 1,300 ambao ni raia wameuawa katika matukio tofauti yanayohusisha makundi ya watu wenye silaha na vikosi vya serikali nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC katika kipindi cha miezi minane iliyopita.

Kwa mujibu wa taaifa hiyo iliyotolewa mjini Geneva Uswis, baadhi ya matukio hayo yanayohusisha mauaji, ukatili na ukiukwaji mwingine wa haki za binadamu huenda yakawa ni uhalifu kwa ubinadamu na uhalifu wa vita.

 Idadi ya waliokumbwa na ukatili huo imeongezeka katika wiki za hivi karibuni wakati machafuko yakishika kasi kwenye majimbo matatu ya Mashariki mwa DRC ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini.

 Ofisi ya haki za binadamu inasema makundi yenye silaha yamefanya mauaji makubwa na uhalifu mwingine na majeshi ya ulinzi na usalama pia yanawajibika kwa ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu katika majimbo hayo matatu lakini pia katika sehemu zingine nchini humo.

Akizungumzia hali hiyo Kamisha mkuu wa ofisi ya haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet amesema “Nimeshtushwa na kuongezeka kwa mashambulio ya kikatili kwa raia wasio na hatia yanayofanywa na makundi yenye silaha,  kuhusu ukiukwaji mkubwa wa haki unaofanywa na vikosi vya ulinzi na usalama ikiwemo mauaji na unyanyasaji wa kingono. Haya sio tu kuwa ni makosa ya jinai lakini pia yanavunja imani miongoni mwa wat una wawakilishi wa serikali wa kiusalama na kisiasa.”

Ameongeza kuwa kwenye jimbo la Ituri kwa mfano kati ya Oktoba Mosi 2019 na Mei 31 2020 raia 531 waliuawa na unyama mkubwa ulitendeka ikiwemo ukatili wa kingono na watu kukatwa vichwa na maiti za watu kukatwa vipandevipande na pande zote makundi yenye silaha na jeshi la Congo FARD na polisi wan chi hiyo PNC wakilaumiwa kuhusika.

Nako Kivu Kaskazini ofisi ya haki za binadamu inasema raia 514 wameuawa kati ya Novemba 2019 na Mei 31 mwaka huu klikihusishwa jeshi la wapiganaji la ADF, jeshi la serikali FARD na jeshi la polisi wa congo la PNC.

Bi Bachlet amesema ulinzi wa rai ani wajibu wa serikali na serikali inapoacha pengo basi waasi wanachukua nafasi. Ameitaka serikali kutimiza wajibu wake chini ya sharia za kimataifa na kuhakikisha wahusika wote wa uhalifu huu wanawajibishwa.