Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNAMID yaongezewa muda Darfur, UNITAMS yazaliwa

UNAMID kwa kushirikiana na Kamati ya Darfur Kaskazini kuhusu wanawake, iliandaa siku moja majadiliano ya azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake, amani na usalama Darfur Kaskazini
UNAMID/Albert González Farran
UNAMID kwa kushirikiana na Kamati ya Darfur Kaskazini kuhusu wanawake, iliandaa siku moja majadiliano ya azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake, amani na usalama Darfur Kaskazini

UNAMID yaongezewa muda Darfur, UNITAMS yazaliwa

Amani na Usalama

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hii leo Alhamis limeuongezea muda Ujumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa Afrika huko Darfur, Sudan, UNAMID na kuweka vigezo mpango utakaofuata unaotegemewa kuanza kazi Januari mosi mwaka ujao wa 2021.

Kwa kutambua uwepo wa ugonjwa wa COVID-19, UNAMID imeongezewa miezi miwili katika majukumu yake na vikosi pamoja na polisi wanaouhudumu kwa sasa watasalia bila kubadilishwa.

UNITAMS yazaliwa

Aidha Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limeanzisha Ujumbe wa pamoja Umoja wa Mataifa wa kusaidia mabadiliko nchini Sudan (UNITAMS) kwa kipidi cha miezi 12 ya kwanza ili kusaidia mchakato wa nchi kuhama kuelekea katika utawala wa kidemokrasia na kuunga mkono ulinzi na ukuzaji wa haki za binadamu na amani endelevu.

UNITAMS pia itasaidia michakato ya amani na utekelezaji wa makubaliano yajayo ya amani; kusaidia ujenzi wa amani, ulinzi wa raia na utawala wa kisheria, hususani katika Darfur na Kusini mwa Kordofan na Blue Nile. 
Pia Baraza limeipa jukumu UNITAMS kusaidia uhamasishaji wa misaada ya kiuchumi na maendeleo na uratibu wa misaada ya kibinadamu. 

Akitoa taarifa kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, tarehe 24 ya mwezi April, Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika idara ya operesheni za amani, Bwana Jean-Pierre Lacroix alisema kuwa hatua zilizochukuliwa kupambana na COVID-19 ikiwemo ufungwaji wa viwanja vya ndege na kusitishwa kwa migao ya vikosi, ilifanya kuwa vigumu kwa UNAMID kuendelea hadi tarehe 31 ya mwezi Oktoba kama ilivyopangwa. 

Miaka 13 ya kuwalinda raia wa Darfur

UNAMID ilianzishwa tarehe 31 Julai mwaka 2007 wakati Baraza lilipoidhinisha azimio namba 1769 la mwaka 2007 kuhusu hali ya Sudan ikiwemo Darfur, kuwalinda raia likiwa kitovu cha shughuli zake.