Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mradi wa sabuni wa wakimbizi wa Mali wawa mkombozi wa COVID-19 Niger:UNHCR

Wanawake wakitengeneza sabuni katika mpango wa CVR huko Bria mpango unaoendeshwa na MINUSCA
MINUSCA
Wanawake wakitengeneza sabuni katika mpango wa CVR huko Bria mpango unaoendeshwa na MINUSCA

Mradi wa sabuni wa wakimbizi wa Mali wawa mkombozi wa COVID-19 Niger:UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Wakimbizi wa Mali nchini Niger wanapambana na janga la virusi vya corona au COVID-19 kwa kutengeneza na kugawa sabuni na dawa ya kutakasa madoa baada ya kupatiwa mafunzo na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR.

Katika kambi yawakimbizi ya Ouallam nchini Niger, kina mama hawa wakimbizi wa Mali wanatengeneza sabuni za maji na za vipande ili waweze kuishi, kazi waliyoianza baada ya kupatiwa mafunzo na shirika la wakimbizi UNHCR.

Kakini sasa kutokana na mlipuko wa janga la corona kazi yao imekuwa muhimu sana katika kusaidia kuzuia maambukizi ya COVID-19. 

UNHCR inasema urahisi wa kupatikana kwa sabuni unachagiza kwa kiasi kikubwa usafi wa mikono na hivyo watu kuweza kujikinga na virusi vya corona.

Mradi huu ni wawanawake wakimbizi ambao wengi walipoteza waume zao vitani na wamesalia na mzigo wa familia , miongoni mwao ni Mariana Amal

“Ni muhimu sana kwetu tuliweza kuanza mradi huu, na tutaendelea nao ili kila mtu aweze kufaidika.”

UNHCR inajitahidi sana kuhakikisha wakimbizi wanajifuza ujuzi mpya ili waweze kujikimu wao wenyewe na familia zao pia. Na kwa sasa sabuni za maji, za vipande na dawa ya kutakatisha madoa zinauzwa si tu kwa wakimbizi wenzao bali pia katika viunga vya mji wa Niamey kwa familia za wenyeji. Mariana anafafanua utaratibu wao

“Mara tu baada ya kutengeneza sabuni hizi tunaziacha zikauke kwa siku moja na kisha tunagawana vipande ili kila mwanamke aende kuuza , na baada ya hapo tunakusanya fedha pamoja.”

Mbali ya kwamba mradi umewawezesha kujikimu UNHCR inasema wanawake hawa wanachangia kwa kiasi kikubwa katika hatua za kiafya na kuhakikisha jamii zao za wakimbizi na wenyeji wanaowahifadhi wako salama.

Hadi sasa UNHCR imeshatoa mafunzo ya kutengeneza sabuni kwa wakimbizi katika makambi ya Hamdallaye, Sayam, Diffa, Tillaberi na Ouallam.