Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waathirika wa mauaji Khartoum bado hawajapata haki mwaka mmoja baadaye:UN

Umati wa watu wakianadamana kwenye mitaa ya mji mkuu wa Sudan Kharthoum 11 Aprili 2019
PICHA:Ahmed Bahhar/Masarib
Umati wa watu wakianadamana kwenye mitaa ya mji mkuu wa Sudan Kharthoum 11 Aprili 2019

Waathirika wa mauaji Khartoum bado hawajapata haki mwaka mmoja baadaye:UN

Haki za binadamu

Wataalam wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa leo wamesema uwajibikaji na haki kwa waathirika wa mashambulizi ya mauaji ya Juni 3 mwaka 2019 dhidi ya watu waliokuwa wakiandamana kwa amani mjini Kharthoum Sudan ni muhimu sana kwa taifa hilo ili kupiga hatua kelekea amani na demokrasia.

“Bado tuna wasiwasi kwamba mwaka mmoja baada ya mashambulizi dhidi watu waliokuwa wakiandamana kwa amani , waathirika na ndugu zao bado wanasubiri haki na mafao” amesema Nyaletsossi Clément Voule, mtaalam wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za uhuru wa kukusanyika na kujumuika. 

Ameongeza kuwa “Hii ni kesi ambayo ni mtihani kwa Sudan. Hatua za kuingia kwenye jamii ya amani na demokrasia hazitokamilika bila kutenda haki na kuwalipa mafao yao waathirika wa kesi hii ambao walipigana kwa ajili ya mapinduzi.”

Wataalam hao wamesema wanatambua kwamba kuanzishwa kwa kamati huru ya kitaifa ya uchunguzi wa madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu katika tukio la 3 Juni mwaka 2019 na kufungua chunguzi zingine kwa uhalifu uliotekelezwa siku za nyuma ni hatua muhimu zilizochukuliwa na mamlaka.

Wamesisitiza kwamba “Wale wote waliohusika ni lazima wawajibishwe bila upendeleo na kwa mujibu wa sharia zilizowekwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.”

Kwa upande wake Aristide Nononsi, mtaalam huru kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Sudan amesema wanawake walikuwa msitari wa mbele wamaandamano hayo ya amani na walikuwa miongoni mwa waathirika wa kwanza wa machafuko, ikiwemo ukiukwaji wa haki za binadamu na ukatili wa kingono.

Wataalam hao wamesema “Tunaitaka tume huru ya kitaifa ya uchunguzi kushughulikia kiwango cha ukatili mkubwa wa kijinsia ambao ulitendeka wakati wa msako wa maandamano hayo na kujitahidi kuhakikisha haki inatendeka na mafao kwa waathirika yanalipwa.”

 Wakiwa wamechochewa na mgogoro wa kiuchumi raia wa Sudan waliandamana kwa amani kwa miezi kadhaa mwaka 2019 maandamano ambayo hatimaye yalipelekea kuondolewa madarakani kwa Rais Al Bashir baada ya kukaa madarakani kwa miaka 30.

Tarehe 3 Juni , vikosi vya usalama vilivyatua risasi katika umati wa waandamanaji waliokuwa wameketi chini na kuwauwa 100 na wengine wengi kujeruhiwa.

“Tunatoa wito kwa mamlaka ya Sudan kutimiza wajibu wao kwa kuanzisha kituo maalum cha waathirika na kuanzisha mchakato wa mpito wa hali za kijinsia kwa ;engo la kushughulikia ukatili wote uliotendeka siku za nyuma, kuzuia usitokee ten ana kuanzisha tume ya mpito ya haki.”

Pia wamesema mabadiliko makubwa yanahitajika kwenye sekta ya ulinzi iku kuweza kuhakikisha uwajibikaji ndani ya mfumo wa kidemokrasia wa kiraia, utawala wa sharia na kuheshimu haki za binadamu.