Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Msaada wahitajika kwa wazazi wakati COVID-19 ikiendelea:UN

Mnamo tarehe 30 Machi, León mwenye umri wa miezi 7 na wazazi wake wakitazama maonyesho ya kila siku ya bandia yaliyowekwa na majirani zao wakati huu wa COVID-19 ili kuburudisha mtoto.
© UNICEF/Javier López Tazón
Mnamo tarehe 30 Machi, León mwenye umri wa miezi 7 na wazazi wake wakitazama maonyesho ya kila siku ya bandia yaliyowekwa na majirani zao wakati huu wa COVID-19 ili kuburudisha mtoto.

Msaada wahitajika kwa wazazi wakati COVID-19 ikiendelea:UN

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Katika kuadhimisha siku ya kimataifa ya wazazi Umoja wa Mataifa umesema msaada unahitajika kwa wazazi ambao wanafanya kazi wakati huu ambapo mlipuko wa janga la virusi vya corona au COVID-19 unaendelea.

Taarifa ya umoja huo iliyotolewa leo imeeleza kwamba “Wazazi wanabeba gharama kubwa za janga la COVID-19. Kama nguzo ya familia na msingi wa jamii zetu wazazi wana wajubu na jukumu la kulinda familia zao dhidi ya madhara ya janga hili, kuhudumia Watoto ambao sasa hawahudhurii shule na wakati huohuo kuendelea kutimiza majukumu ya kazi zao. Bila msaada kutoka kwa wazazi afya ya Watoto, elimu na usatawi wao utakuwa hatarini.”

Hivyo Umoja wa Mataifa umesisitiza kwamba kwa kuanzisha sera Rafiki kwa familia makazini, makampuni na mashirika yatakuwa katika nafasi nzuri ya kuchagiza usalama wa waatoto na ustawi na pia kutoa msaada unaohitajika kwa wafanyakazi.

Na wakati huu janga hilo la COVID-19 likiendelea mashirika ya Umoja wa Mataifa likiwemo la kuhudumia Watoto UNICEF, la kazi ILO na la kushughulikia masuala ya wanawake UN Women yamesema sera Rafiki kwa familia na hatua zingine zitakazosaidia katika mazingira ya kazi ni muhimu sana katika kuzisaidia familia zenye wazazi wanaofanyakazi katika kupunguza athari mbaya za janga hili kwa watoto.

Historia ya siku ya wazazi

Siku ya kimataifa ya wazazi huadhimishwa kila mwaka Juni Mosi na tangu miaka ya 1980, umuhimu wa jukumu la familia ulionekana kuongezeka kwa jumuiya ya kimataifa na ndipo Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa likaamua kupitisha azimio na kuutangaza mwaka huo kuwa mwaka wa familia na pia kutangaza siku ya familia.

Lakini mwaka 2012 ndipo Baraza la Kuu lilipopitisha siku ya kimataifa ya wazazi kwa lengo la kusisitiza jukumu muhimu la wazazi katika malezi ya watoto.

 

Wazazi wakiwa na uhakika wa tiba na chanjo kwa watoto wao, nao pia wanaweza kushiriki kwenye shughuli za kujikwamua kiuchumi. Hapa ni Sierra Leone watoto wakipatiwa chanjo dhidi ya Polio.
UNICEF/Kate Holt
Wazazi wakiwa na uhakika wa tiba na chanjo kwa watoto wao, nao pia wanaweza kushiriki kwenye shughuli za kujikwamua kiuchumi. Hapa ni Sierra Leone watoto wakipatiwa chanjo dhidi ya Polio.

Siku hii inatambua kwamba familia inajukumu muhimu kwa kukuza na kuwalinda Watoto kwa ajili ya maendeleo yao na mustakabali wao, na kusisitiza kwamba watoto wanapaswa kukua katika mazingira ya familia na mazingira ya furaha, upendo na uelewa.

Baraza kuu likipitisha azimio la kuanzisha siku ya kimataifa ya wazazi lilisema “Siku ya wazazi inatoa fursa ya kuwatambua wazazi wote kwa wajibu wao kwa Watoto na kujitolea Maisha yao yote kuimarisha uhusiano huu.”