Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu wawili wapoteza maisha na maelfu makazi yao baada ya moto kuzuka kambini Nigeria:UNHCR

Wakimbizi kutoka Nigeria wakiwasili katika kijiji cha Goura nchini Cameroon mwezi Januari 2019
UN Photo/Eskinder Debebe)
Wakimbizi kutoka Nigeria wakiwasili katika kijiji cha Goura nchini Cameroon mwezi Januari 2019

Watu wawili wapoteza maisha na maelfu makazi yao baada ya moto kuzuka kambini Nigeria:UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR na wadau wengine wa misaada ya kibinadamu wanaoneza juhudi za misaada kwa ajili ya watu 4,000 ambao ni wakimbizi wa ndani waliopoteza kila kitu katika moto mkubwa uliozuka na kuteketeza kambi ya wakimbizi wa ndani mjini Maiduguri jimbo la Borno Mashariki mwa Nigeria.

Akizungumza na waandishi wa Habari kwa njia ya mtandao mjini Geneva Uswiss hii msemaji wa UNHCR Shabia amesema “Moto huo uliozuka katika mkesha wa sherehe za Eid-el-Fitr wakati wa kuhitimisha mfungo wa Ramadhan umekatili Maisha ya watu wawili na kuacha mamia ya familia bila makazi  katika kambi hiyo inayohifadhi wakimbizi wa ndani 40,000. Moto huo ulianza kutokana na kusambaa kwa cheche kutoka jikono na hivyo kuwasha moto ambao baada ya muda mfupi ulizingira makazi yote ya kambi. Nyumba ziliteketea kabisa na kuunguza pia majengo mengine na wathirika wakubwa ni wanawake.”

Ameogeza kuwa karibu watu 300,000 wakimbizi wa ndani wamewekwa katika makazi maalum mjini Maiduguri mji mkuu wa jimbo la Borno.  Katika miezi michache iliyopita matukio kadhaa ya moto yametokea katika makambi ya wakimbizi wa ndani kote kaskazini Mashariki mwa Nigeria ambako makazi ya wakimbizi wa ndani yako karibukaribu sana ukizingata masuala ya usalama.

UNHCR yahakikisha msaada kwa wakimbizi

Shirika la UNHCR limesema linafanyakazi na mamlaka, mashirika ya misaada na wadau wengine wa eneo hilo kuhakikisha kwamba wakimbizi walioathirika wanapata malazi na misaada mingine muhimu kwa kuwa kwa mara nyingine watu wametawanywa ndani nan je ya kambi.

Kwa mujibu wa UNHCR hivi sasa watu wengi walioathirika wakiwemo Watoto wanaishi katika maeneo ya wazi nje huku wakihitaji msaada wa haraka wa malazi, chakula na nguo.

Watu waliotawanywa ziwa Chad

Jumla ya watu milioni 2.5 wametawanywa katika eneo la ziwa Chad, wakiwemo milioni 1.8 ndani ya Nigeria na waliosalia wako nchini Cameroon na Chad.

Kukiwa na machafuko ya Boko Haram yanayoendelea na wapiganaji wa makundi mengine , maelfu ya watu wengine zaidi wanalazimika kukimbia kila siku kuokoa maisha yao.

Wakati huhuo shirika la UNHCR linasema wasichana, wanawake na wahudumu wa misaada wanaendelea kubeba gharama ya machafuko hayo.

Na waakati machafuko hayo yakiongezeka tishio la janga la virusi vya corona au COVID-19  limeleta tishio jipya kwa wakimbizi wa ndani  ambao wanaishi katika makazi na makambi yaliyofurika watu ambako hatua za kujitenga ni mtihani mkubwa  na haziwezekani.

Katika kukabiliana na hali hiyo UNHCR inashirikiana na shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP kupanua makambi kadhaa na kujenga malazi mengine ya ziada.