Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chonde chonde Burundi weka mazingira salama kwa uchaguzi mkuu- AU, UN

Watoto wanajaza maji katika vikombe. HDI yasema  watoto hawa wanaweza kukaa shelen mda mdogo kuliko wenzao katika mataifa yaliyoendelea..
UNICEF/UNI180029/Colfs
Watoto wanajaza maji katika vikombe. HDI yasema watoto hawa wanaweza kukaa shelen mda mdogo kuliko wenzao katika mataifa yaliyoendelea..

Chonde chonde Burundi weka mazingira salama kwa uchaguzi mkuu- AU, UN

Haki za binadamu

Kuelekea uchaguzi mkuu nchini Burundi Jumatano wiki hii, Muungano wa Afrika, AU, na Umoja wa Mataifa wametoa wito kwa mamlaka nchini humo zihakikishe kuna mazingira salama kwa raia kuweza kupiga kura.
 

Taarifa ya pamoja ya vyombo hivyo iliyotolewa hii leo imesema wamekuwa wakifuatilia kwa karibu kampeni za uchaguzi na wanasalia na hofu ya ripoti za ukandamizaji na ghasia kati ya wafuasi wa pande kinzani.
“UN na AU wanashawishi pande husika katika maandalizi ya uchaguzi wa Mei 20, 2020 nchini Burudndi, vikosi vya ulinzi na usalama na vyombo vya habari vinavyomilikiwa na serikali kuchangia vyema katika kulinda mazingira ya utulivu na amani kwa ajili ya uchaguzi huru, wa haki, jumuishi, wazi na halali nchini Burundi,” imesema taarifa hiyo.

Halikadhalika imesihi wanasiaasa wajizuie katika vitendo vyovyote vya ghasia na kauli za chuki na badala yake washiriki kwenye mazungumzo ya kuwezesha kufanyika kwa chaguzi huru na za amani.

Muungano na Afrika na Umoja wa Mataifa pia wamesihi mamlaka nchini Burundi zihakikishe kuwa zinaweka mazingira ili wanawake nao waweze kushiriki kwa ukamilifu kwenye mchakato mzima wa uchaguzi.

Kwa upande wa vyama vya siasa, kamisheni  ya AU na sekretarieti ya UN zimeviomba vizingatie kanuni za maadili ambazo walitia saini mwezi Desemba mwaka jana.

Vile vile wameombwa wazingatia kanuni za kulinda raia wake dhidi ya ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19.

Wiki iliyopita, Kamisheni ya uchunguzi ya UN ilionesha wasiwasi wake juu ya ongezeko la ghasia na ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Burundi wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu.

Pande mbili hizo pia zimeelezea kusikitishwa kwake na hatua ya serikali ya Burundi ya kuwafukuza nchini humo wafanyakazi wanne wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO, akiwemo mwakilishi wake.