Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mafuriko, mapigano, nzige, COVID-19 Somalia, wakimbizi wa ndani hatarini - UNHCR

Wanawake wakiteka maji katika mradi wa maji uliofadhiliwa na shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa, IOM katika kambi ya wakimbizi wa ndani ya Dolow nchini Somalia. IOM, WFP na mashirika mengine waliweze kusaidia mahitaij ya wakimbizi hao kutokana na mfu
WFP/Georgina Goodwin
Wanawake wakiteka maji katika mradi wa maji uliofadhiliwa na shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa, IOM katika kambi ya wakimbizi wa ndani ya Dolow nchini Somalia. IOM, WFP na mashirika mengine waliweze kusaidia mahitaij ya wakimbizi hao kutokana na mfuko wa CERF.

Mafuriko, mapigano, nzige, COVID-19 Somalia, wakimbizi wa ndani hatarini - UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Mafuriko makubwa, mizozo, nzige wa jangwani, uchumi uliodhoofika na janga la ugonjwa wa virusi vya Corona, au COVID-19, vinatishia usalama na ustawi wa wakimbizi wa ndani milioni 2.6 nchini Somalia. 

Msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR, Charles Yaxley akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya video hii leo amesema kuwa, ni kwa kuzingatia hali hiyo “UNHCR inahofia vitisho hivyo vinaweza kuleta madhara makubwa linatoa wito wa kuchukuliwa kwa hatua za pamoja za jamii ya kimataifa na kitaifa ili kukidhi mahitaji  ya sasa ya kibinadamu nchini humo.”

UNHCR inasema kuwa tangu mwanzoni mwa mwaka huu, zaidi ya wasomali 220,000 wamejikuta wakimbizi wa ndani, ambao kati yao hao, 136 wamekimbia makazi yao kutokana na mzozo.

Sababu nyingineni pamoja na ukame uliosababisha watu washindwe kuendelea na shughuli za kujipatia kipato pamoja na mafuriko.

Mama akinunua samaki wa mkebe kwa vocha cha WFP Burao, Kaskazini mwa Somalia.
WFP/C. McDonough
Mama akinunua samaki wa mkebe kwa vocha cha WFP Burao, Kaskazini mwa Somalia.

Bwana Yaxley amesema kuwa "katika maeneo ya kusini na kati mwa Somalia, mafuriko yaliyosababishwa na mvua za ghafla pamoja na mvua za msimu, vimeshafurusha watu 90,000 na wengine zaidi wanatarajiwa kukimbia makwao na hivyo kufanya hali ya wakimbizi wa ndani kuwa mbaya zaidi kutokana na masaibu ambayo tayari yanawakabili.”
 

Mapema wiki hii, UNHCR na serikali ya Somalia walisafirisha misaada ya dharura ikiwemo sabuni, blanketi, matandiko, vifaa vya jikoni ili kusaidia wakazi wa  maeneo ya Baidoa, Bardheere na Qardho. 

Shehena ya pili imepelekwa leo kwenye miji ya Qardho, Bardheere, Beletweyn, na Berdale ikilenga kufikia watu 37,000.

Mzozo ni upi Somalia

Mwezi Machi na Aprili mwaka huu, operesheni za kijeshi dhidi ya kikundi cha Al Shabab zilianza upya kwenye maeneo ya Shabelle Chini na hivyo kulazimisha watu zaidi  ya 50,000 wakimbie makwao.

“Wakazi wa eneo hilo walikabiliana moja kwa moja na milio ya risasi na mashambulio ya makombora yaliyoelekezwa kwenye vijiji vyao huku pia wakikumbana na milipuko barabarani. Utumikishaji wa watoto, ubakaji, ukatili wa kingono na watu kukamatwa kiholela navyo pia vimeripotiwa,”  amesema Bwana Yaxley.

Wakimbizi wa ndani na COVID-19

UNHCR inaamini kuwa hali ya kibinadamu inazidi kudorora wakati huu wa janga la COVID-19 linavyozidi kusambaa, ambapo “wakimbizi wa ndani milioni 2.6 nchini Somalia wanaishi kwenye makazi yaliyojaa kupita kiasi, hususan wakimbizi wapya ambao wanahamahama wakiwa na virago vyao kwenye mifuko ya plastiki.”

Shirika hilo linasema hali ya kutochangahamana haiwezekani, hakuna maji salama ya kunywa wala kunawa na mazingira ni rafiki zaidi kwa virusi vya Corona kuenea.

Hata hivyo UNHCR imepongeza hatua za serikali ya Somalia za kuanzisha upimaji wa virusi vya Corona nchini kote, ingawa inasema kuwa, ina hofu kuwa udhoofu wa mifumo ya afya kutokana na miongo ya mapigano na uhaba wa vifaa vya kuchunguza virusi vya Corona duniani, vinaweza kukwamisha ari ya kukabilia Corona.

Nchini Somalia licha ya kuwepo wagonjwa 928 nchini kote, katika kambi za wakimbizi wa ndani kumepatikana mgonjwa 1 pekee.