Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Miongozo mipya yatolewa kuhusu njia ya ufunguzi salama wa shule hali itakapotengamaa

Mtoto wa Miaka Saba Francesca(sio jina sahihi)akipata matibabu kutoka kwa Daktari Antonella Tonchiaro ktika makazi yasio rasmi anapo ishi Rome nchini Italy.Daktari Tochiaro ni mmoja wa wafanyikazi wa INTERSOS/UNICEF.
© UNICEF/Alessio Romenzi
Mtoto wa Miaka Saba Francesca(sio jina sahihi)akipata matibabu kutoka kwa Daktari Antonella Tonchiaro ktika makazi yasio rasmi anapo ishi Rome nchini Italy.Daktari Tochiaro ni mmoja wa wafanyikazi wa INTERSOS/UNICEF.

Miongozo mipya yatolewa kuhusu njia ya ufunguzi salama wa shule hali itakapotengamaa

Afya

Mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO, la kuhudumia watoto UNICEF kwa kushirikiana na Benki ya dunia, hii leo mjini New York Marekani, Paris Ufaransa na Roma Italia, wametoa miongozo kuhusu namna salama ya kuzifungua shule kutokana na kufungwa ambako kunawaathiri takribani wanafunzi bilioni 1.3 kote duniani.

Mashirika hayo pia yameonya kuwa kufungwa kwa taasisi za elimu katika harakati za kupambana na janga la COVID-19 kunaleta hatari kubwa kwa elimu na ustawi wa watoto hususani kwa wale watoto waliotengwa mbali ambao wanategemea shule kwa ajili ya elimu, afya, usalama na lishe. Miongozo hiyo inatoa ushauri kwa mamlaka za kitaifa na kijamii kuhusu jinsi ya kuwalinda watoto kwa usalama wakati wanaporejea shuleni.

Balozi wa amani akizungumza na wanafunzi katika shule mjini Kinshasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC , kuhusu kuchagiza amani na usawa wa kijinsia
MONUSCO/Dominique Cardinal
Balozi wa amani akizungumza na wanafunzi katika shule mjini Kinshasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC , kuhusu kuchagiza amani na usawa wa kijinsia

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF, Henrietta Fore, anasema, “ongezeko la kukosekana kwa usawa, matokeo ya afya duni, ajira kwa watoto na ndoa za utotoni ni baadhi tu ya matishio ya muda mrefu kwa watoto ambao wanaikosa shule. Tunafahamu kuwa watoto wanavyokaa nje ya shule kwa muda, ndivyo ambavyo kuna uwezekano mkubwa wa kutorejea shuleni. Isipokuwa tutoe kipaumbele katika kuzifungua shule, itakapokuwa salama kufanya hivyo, tutashuhudia kurejea nyuma kwa kiasi kikubwa ukuaji wa elimu.”

Mwongozo mpya unaeleza kwamba wakati bado hakuna ushahidi wa kutosha kupima matokeo ya kufungwa kwa shule  kufungwa kwa shule kulinganisha na maambukizi, athari mbaya za kufungwa kwa shule kwa usalama wa watoto zimeandikwa vizuri.  Faida zilizopatikana katika kuongeza ufikiaji wa elimu ya watoto katika miongo ya hivi karibuni iko katika hatari ya kupotea na katika mazingira mabaya zaidi, kurejea nyuma kabisa.

Wakati nchi zinatafakari ni lini zifungue shule, UNESCO, UNICEF, WFP na Benki ya dunia, kama sehemu ya ushirikiano wa kimataifa, wanazisihi serikali kutathmini faida za masomo katika mazingira ya darasa ikilinganishwa na kusoma nje ya mazingira hayo na hatari zinazohusiana na kufungua tena shule ikizingatiwa ushahidi usio wazi kuhusu hatari za kuambukizwa inayohusiana na mahudhurio shuleni.

Miongozo mipya iliyotolewa ni pamoja na kuangaliwa suala la marekebisho ya sera, ufadhili, kuendesha masomo kwa usalama kwa kuhakikisha kunakuwa na mazingira ya kudhibiti mambukizi, kujikita katika kufidia masomo yaliyopotea na kuwafikia wanafunzi walioko mbali au katika makundi duni ya mazingira yasiyofikika kirahisi.