Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waajiri waaswa kuwalinda wafanyakazi wakati na baada ya COVID-19: ILO

Huachao Sang,Daktari kutoka wilaya ya Jiangsu akitafuta karatasi za mgonjwa wake katika hospitali ilioko Wuhan.
Sang Huachao
Huachao Sang,Daktari kutoka wilaya ya Jiangsu akitafuta karatasi za mgonjwa wake katika hospitali ilioko Wuhan.

Waajiri waaswa kuwalinda wafanyakazi wakati na baada ya COVID-19: ILO

Afya

Shirika la kazi dunini ILO limeonya kwamba bila mikakati bora ya kuwalinda wafanyakazi wakati watakaporejea kazini baada ya hatua za kutochangamana , kuna uwezekano mkubwa wa wimbi la pili la mlipuko wa janga la corona au COVID-19.

 Shirika la kazi dunini ILO limeonya kwamba bila mikakati bora ya kuwalinda wafanyakazi wakati watakaporejea kazini baada ya hatua za kutochangamana , kuna uwezekano mkubwa wa wimbi la pili la mlipuko wa janga la corona au COVID-19.  

Onyo hilo limetolewa leo na ILO katika ujumbe wake wa siku ya kimataifa ya usalama na afya kazini wakati huu ambapo shinikizo linaongezeka la kutaka kulegezwa vikwazo vya watu kusalia majumbani.

Limetoa wito kwa serikali kuchukua hatua kuzuia na kudhibiti COVID-19 katika sehemu za kazi, likichagiza ushiriki na majadiliano baina ya wafanyakazi na mashirika yaliyowaajiri.

Akifafanua kuhusu hatua hizo za kuwalinda wafanyakazi Monica Gachuki mtafiti wa masuala ya ajira wa ILO amesema

“Mosi ni kupanga, kuweka sera na mikakati, pili kutathimini hatari na mawasiliano, tatu hatua za kuzuia na kukabiliana na janga hilo kazini, nne utaratibu maalum kwa ajili ya wagonjwa wanaoshukiwa na waliothibitishwa, na miwsho janga kama COVID-19 linaweza kusababisha kiwango kikubwa cha msongo kwa watu wote hivyo hatua za usalama zinapaswa kutekelezwa kupunguza hatari za athari za kisaikolojia na kuchagiza afya ya akili na ustawi wa wafanyakazi.”

Naye mkurugenzi mkuu wa ILO Guy Ryder  amesema  usalama na afya ya wafanyakazi ndio kipaumbele leo hii, wakati wa mlipuko wa magonjwa ya kuambukiza na  jinsi gani tunaweza kuwalinda wafanyakazi  wetu ni dhahiri inategemeana na jinsi gani jamii zetu ziko salama na jinsi gani biashara zetu zitakuwa na mnepo wakati mlipuko huu ukiendelea.

Amesisitiza kwamba “Ni kwa kutekeleza mikakati ya usalama na afya ndivyo tutakavyoweza kulinda maisha ya wafanyakazi , familia zao na jamii kwa ujumla kwa kuhakikisha kazi inaendelea na uchumi hauyumbi.”

Na kwa wafanyakazi walio msitari wa mbele amesema kunapaswa kuchukulia hatua kulingana na mahitaji yao wakiwemo wahudumu wa afya, wauguzi, madaktari na wahudumu wa dharura, pia wale wanaofanyakazi kwenye maduka ya chakula na huduma za usafi.