Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za binadamu ziwe muongozo wa vita dhidi ya COVID-19:UN

Katibu Mkuu Antonio Guterres akitoa ujumbe kuhusu Janga la COVID-19.
UN Photo/Eskinder Debebe)
Katibu Mkuu Antonio Guterres akitoa ujumbe kuhusu Janga la COVID-19.

Haki za binadamu ziwe muongozo wa vita dhidi ya COVID-19:UN

Haki za binadamu

Umoja wa Mataifa umesisitiza kwamba haki za binadamu zinapaswa kuwa muongozo katika hatua zinazochukuliwa kupambana na janga la mlipuko wa virusi vya corona au COVID-19.

Umoja wa Mataifa umesisitiza kwamba haki za binadamu zinapaswa kuwa muongozo katika hatua zinazochukuliwa kupambana na janga la mlipuko wa virusi vya corona au COVID-19.

Katika ujumbe wake maalum uliotolewa leo kuhusu haki za binadamu na janga la COVID-19 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema “Sisi sote tuko katika janga hili kwa Pamoja, Janga la COVID-19 ni dharura ya afya ya umma lakini ni zaidi hivyo. Ni janga la kiuchumi, kijamii na la kibinadamu ambalo lina hatari ya kuwa janga la haki za binadamu.”

Amekumbusha kuwa mnamo mwezi Februari, alizindua wito wa kuchukua hatua ili kuweka hadhi ya kibinadamu na ahadi ya Azimio la Haki za Binadamu katika msingi wa kazi yetu.

 

Sisi sote tuko katika hili kwa pamoja: Haki za Binadamu na kupambana na COVID-19-Guterres

 

“Kama nilivyosema wakati huo, haki za binadamu haziwezi kuwa za kutopewa kipaumbele katika nyakati za shida  na sasa tunakabiliwa na janga kubwa zaidi la kimataifa katika vizazi kadhaa.”

Guteres amesema leo, anatoa ripoti inayoangazia jinsi haki za binadamu zinavyopaswa kuwa kipaumbele katika kupambana na COVID-19.

“Ujumbe uko wazi, watu na haki zao lazima viwekwe mbele na katikati, Kurunzi ya haki za binadamu inaweka kila mtu kwenye picha na inahakikisha kwamba hakuna mtu anayeachwa nyuma. Majibu ya haki za binadamu yanaweza kusaidia kulipiga gonjwa la COVID-19, kwa kuweka umakini juu ya umuhimu wa huduma ya afya kwa kila mtu.”

 Janga la COVID-19 halibagui nasi tusifanye hivyo

Ameongeza kuwa majibu hayo pia yanatumika kama mfumo muhimu wa onyo la kuonesha ni nani anaathirika zaidi, kwa nini, na nini kifanyike juu yake.

“Tumeona jinsi virusi ambavyo havibagui, lakini athari zake zinabagua kuweka wazi udhaifu mkubwa katika utoaji wa huduma za umma na kutokuwepo kwa usawa wa muundo ambao unazuia ufikiaji wa huduma hizo. Lazima tuhakikishe haya yanashughulikiwa vizuri katika majibu.”

Katibu Mkuu ameongeza kuwa zinashuhudiwa athari kubwa zaidi kwa jamii fulani, kuongezeka kwa kauli za chuki, kulengwa kwa vikundi vilivyo katika mazingira hatarishi, na hatari za hatua kali za usalama zinazodhoofisha mwitikio wa kiafya.

Pamoja na kuongezeka kwa utaifa wa kujitenga, udikteta na harakati dhidi ya haki za binadamu katika nchi zingine, janga linaweza kutoa kisingizio cha kuchukua hatua za kukandamiza kwa sababu zisizohusiana na janga hili.

Hali hii haikubaliki

Bwana Guterres amesisitiza kuwa “Hii haikubaliki na zaidi kuliko wakati mwingine wowote, serikali lazima ziwe na uwazi, zenye kuchukua hatua na zinazowajibika. Raia na uhuru wa vyombo vya habari ni muhimu. Mashirika ya asasi za kiraia na sekta binafsi wana majukumu muhimu ya kutekeleza.”

Na kisha amekumbusha kwamba “katika yote tunayofanya, hebu na tusisahau kamwe kwamba tishio ni virusi, sio watu. Lazima tuhakikishe kuwa hatua zozote za dharura pamoja na hali ya dharura ni za kisheria, zenye uwiano, muhimu na sio za kibaguzi, zinalenga jambo na muda mahususi, na kuchukua njia zinazofaa kulinda afya ya umma.”

Jawabu muafaka

Katika hilo mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amesema jibu bora ni lile ambalo hujibu sawasawa vitisho vya haraka wakati linalinda haki za binadamu na utawala wa sheria.

Kwa kuangalia mbele, asemema tunahitaji kujiimarisha vizuri. Malengo ya Maendeleo Endelevu ambayo yametekelezwa na haki za binadamu yanatoa mfumo wa uchumi unaojumuisha na jamii endelevu.

Amesisitiza kwamba kuimarisha uchumi na haki za jamii inaimarisha ustahilivu wa muda mrefu.

Na katika kujikwamua na janga hili Guterres amesema “Kurejea katika hali nzuri pia lazima kuheshimu haki za vizazi vijavyo, kuongeza hatua ya mabadiliko ya tabianchi inayolenga kudhibiti hewa ya ukaa ifikapo mwaka 2050 na kulinda bianuwai. Sote tumo katika hili pamoja. Virusi vinatishia kila mtu,lakini haki za binadamu humwinua kila mmoja.”

Mwisho amesema “Kwa kuheshimu haki za binadamu katika wakati huu wa janga, tutaunda suluhisho bora na la pamoja kwa dharura ya leo na kupona kwa kesho.”