Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ni wajibu wetu kuwalinda Watoto wakati huu wa COVID-19

Watoto wa chekechea wakiwa wamevaa barakoa mjini Johannesburg nchini Afrika Kusini wakati huu wa COVID-19
© UNICEF/Shiraaz Mohamed
Watoto wa chekechea wakiwa wamevaa barakoa mjini Johannesburg nchini Afrika Kusini wakati huu wa COVID-19

Ni wajibu wetu kuwalinda Watoto wakati huu wa COVID-19

Afya

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo ametoa wito wa kuwalinda Watoto wakati huu mlipuko wa janga la virusi vya corona au COVID-19 ukisambaa kote duniani na kushuhudiwa mwenendo unaotia hofu.

Katika ujumbe wake kwa vyombo vya Habari kupitia njia ya mtando mjini New York Marekani Guterres amesema “masikini na watu wasiojiweza katika jamii ndio walioathirika vibaya na janga hili na pia hatua za kukabiliana nalo na hasa

wasiwasi mkubwa juu ya ustawi wa watoto wa dunia hii. Tunashukuru kwamba hadi sasa hawajaathirika kwa kiasi kikubwa na dalili mbaya za maradhi haya.

Lakini maisha yao yameathirika kabisa. Ninatoa wito kwa familia kila mahali na viongozi katika kila ngazi, walindeni watoto wetu.”

Hatari zinazowakabili watoto
 

Katibu mkuu amesema leo wamezundua ripoti inayoangazia hatari kubwa nne zinazowakabili Watoto.

 

Kwanza elimu: Karibu watoto wote hivi sasa hawapo shuleni na shule zingine zinatoa masomo ya kusomea mbali lakini haya hayaparikani kwa wote hivyo amesema watoto walio katika nchi ambazo huduma hizo za mtandao ni haba na za gharama wanapata shida sana.

Pili chakula: Amesema watoto milioni 310 wa shule karibu nusu ya watoto wote duniani wanategemea shule kama chanzo cha kawaida cha lishe ya kila siku.

Hata kabla ya janganga la COVID-19 ulimwengu ulikabiliwa na viwango visivyokubalika vya utapiamlo na kudumaa kwa watoto.

Tatu, usalama: Wakati watoto wakiwa nje ya shule, familia zao katika amri ya kutotembea na mdororo wa uchumi ukishika kasi , viwango vya mfadhaiko wa familia vinaongezeka.

Amesema watoto wote ni waathirika na mashuhuda wa dhuluma za majumbani na ukatili.

Na huku shule zikiwa zimefungwa njia muhimu ya tahadhari ya mapema haipo hivyo kuna hatari pia kwamba wasichana wataacha shule na kusababisha ongezeko la mimba za utotoni.

Guterres amesisitiza kwamba “hatupaswi kupuuza ongezeko la hatari zinazowakabili watoto wakati wakitumia muda mwingi mtandaaoni. Hii inaweza kuwaacha watoto katika hatari ya ufundishwaji na unyanyasaji wa kingono mtandaoni.”

Ameongeza kuwa ukosekana kwa mawasiliano ya moja kwa moja na marafiki na wenza kunaweza kusababisha kuongezeka kwa hatari kama vile kutuma picha za ngono.

Pia kuongezeka kwa wakati na kutokuwa na mpangilio mtandaani kunaweza kuwaweka watoto kwenye madhara na vurugu kama vile hatari kubwa ya uonevu mtandaoni.

Amesisitiza kwamba “Serikali na wazai wote wanajukumu la kuhakikisha watoto wako salama. Makampuni ya mitandao ya kijamii yana wajibu maalum wa kuwalinda walio hatarini.”

Nne, afya : amesema mapato ya kaya yanayopunguzwa yatalazimisha familia masikini kupunguza matumizi muhimu ya kiafya na chakula yanayoathiri hususani watoto, wanawake wajawazito na kina mama wanaonyonyesha.

Mbali ya hayo amesema hivi sasa “Kampeni ya chanjo ya polio imesitishwa, kampeni za chanjo za surau zimesitishwa kwa angalau nchi 23. Na wakati mifumo ya afya ikilemewa, watoto wagonjwa inakuwa vigumu kupata fursa ya huduma.”

 

Matokeo kwa watoto

Muuguzi akichunguza joto ya mtoto katika kituo cha afya Beirut, Lebanon wakati huu wa mlipuko wa COVID-19
© UNICEF/Fouad Choufany
Muuguzi akichunguza joto ya mtoto katika kituo cha afya Beirut, Lebanon wakati huu wa mlipuko wa COVID-19

 

Pia ameweka bayana kwamba wakati mdororo wa uchumi ukishika kasi duniani kuna uwezekano wa maelfu ya vifo zaidi vya watoto mwaka 2020.

Haya ni baadhi tu ya matokeo ya ripoti tunayotoa leo na hitimisho lake liko bayana. “Lazima tuchukue hatua sasa kwa kila moja ya vitisho hivi kwa watoto wetu. Viongozi lazima wafanye kila wawezalo kwa uwezo wao kupunguza athari za majanga.”

Amesema kile kilichoanza kama dharura ya afya ya umma kimegeuka kuwa mtihani mkubwa kwa ahadi ya ulimwengu ya kutomuacha yeyote nyuma.

Ripoti inahimiza serikali na wahisani kuweka kipaumbele kwa elimu ya watoto wote.

Inapendekeza watoe msaada wa kiuchumi, ikiwemo uhamishaji wa fedha kwa familia zenye kipato cha chini na kupunguza usumbufu kwa huduma za kijamii na za afya kwa watoto.

“Lazima tutoe kipaumbele kwa wasiojiweza zaidi, watoto walio katika mazingira ya vita, Watoto wakimbizi, na waliotawanywa na watoto wanaoishi na ulemavu.”

Mwisho Guterres amesema “lazima tuahidi kujijenga vyema zaidi baada ya kujikwamua kutokana na janga la COVID-19, ili kuhakikisha tuna uchumi endelevu na jumuishi na jamii inayokwenda sanjari na malengo ya maendeleo endelevu. Na janga hili likiwaweka Watoto wengi hatarini duniani , narejea ombi langu la haraka , hebu tuwalinde Watoto wetu na kulinda ustawi wao.”