Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tulichojifunza kuhusu Ebola chaweza kusaidia vita dhidi ya COVID-19:Dkt. Moeti

UNICEF inaunga mkono juhudi za serikali nchini DRC kukabiliana na COVID-19 ambapo wamechapisha vifaa vya kutoa elimu kwa lugha mbali mbali.
© UNICEF/UNI314617/Desjardins
UNICEF inaunga mkono juhudi za serikali nchini DRC kukabiliana na COVID-19 ambapo wamechapisha vifaa vya kutoa elimu kwa lugha mbali mbali.

Tulichojifunza kuhusu Ebola chaweza kusaidia vita dhidi ya COVID-19:Dkt. Moeti

Afya

Juhudi kubwa zikiendelea kote duniani kupambana na mlipuko wa virusi vya Corona au COVID 19, barani Afrika idadi ya wagonjwa inaendelea kuongezeka na Kwa mujibu wa mkurugenzi wa shirika la afya duniani WHO kanda ya Afrika Dkt. Matshidiso Moeti.

Changamoto ni kubwa barani humo katika kupambana na COVID-19 lakini yale waliyojifunza kuhusu Ebola yanaweza kusaidia hasa katika kuishirikisha jamii,“Nadhani ni muhimu kuanzia katika kiwango cha watu binafsi majumbani kwao, tulichojifunza kutokana na mlipuko wa Ebola ambacho tunakifanya sasa ni jinsi gani ya kuanza kuchukua hatua mapema katika ngazi ya jamii, kwa sababu jamii inaweza kuwa muhimu sana hata katika mwanzo wa mlipuko kama ufuatiliaji na kutambua mwenendo wa ugonjwa. Tumejifunza pia kwamba ni muhimu sio tu kuwaambia watu vitu pia kusikiliza na kujumuisha maoni yao katika mikakati yetu”

Ameongeza kuwa ni muhimu kuachana na dhana potofu na kuhakikisha yaliyotokea kwa Ebola hayatokei kwa COVID-19, “Kuna taarifa nyingi sana na baadhi si sahihi ambazo zinazunguka kuhusu mlipuko wa virusi hivi. Hivyo tunafahamu kwamba ni muhimu sana kama tulivyojifunza kutokana na Ebola kuifikia jamii na taarifa sahihi, sio tu kuwapa ujumbe wa radio , bali kuzungumza na watu, kuwasikiliza na kubadili mikakati yetu kutokana na hayo. Pia tumepata uzoefu wa mioundombinu ya Ebola ambayo tayari iilikwishawekwa”