Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kufuatia mlipuko wa COVID-19 mkutano wa COP26 waahirishwa:UN

Mkutano wa 26 wa kimataifa wa mbadiliko ya tabianchi COP26 uliokuwa ufanyike baadaye mwaka huu umehairishwa.
Unsplash/Adam Marikar
Mkutano wa 26 wa kimataifa wa mbadiliko ya tabianchi COP26 uliokuwa ufanyike baadaye mwaka huu umehairishwa.

Kufuatia mlipuko wa COVID-19 mkutano wa COP26 waahirishwa:UN

Afya

Umoja wa Mataifa umetangaza kuahirishwa kwa mkutano wa 26 wa kimataifa wa mbadiliko ya tabianchi COP26 uliokuwa ufanyike baadaye mwaka huu kutokana na janga la kimataifa la virusi vya Corona , COVID-19.

Kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Msataifa Antonio Guterres amesema anaunga mkono maamuzi ya serikali ya Uingereza na ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na masuala ya mabadiliko ya tabianchi UNFCCC ya kuchelewesha mkutano huo wa COP26, ambao ulikuwa ufanyike mwezi Novemba mwaka huu mjini Glasgow.

Guterres amesema “wakati maelfu ya watu wmeambukizwa na kuugua COVID-19 haja ya kuudhibiti ugonjwa huo na kulinda maisha ya watu ndio kipaumbele chetu cha kwanza.”

Katibu Mkuu amesisitiza kwamba “Ni lazima tuendelee na juhudi zetu na hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi hususan wakati nchi zinachukua hatua za kujikwamua kutoka kwenye janga hili”.

Amesisitiza kuwa sayansi kuhusu mabadiliko ya tabianchi haijabadilika uchafuzi wa hali ya hewa sasa umefikia kiwango cha juu san ana athari zake zinaongezeka na zitaongeza athari za kijamii na kiuchumi zinazosababishwa na janga hili la corona.

Guterres amesema janga hili la Corona linasisitiza umuhimu wa sayansi na ushahidi kuzijulisha sera na maamuzi ya serikali . Sayansi imeweka bayana kwamba tabia za binadamu zinavuruga mfumo wa uwezo wa kawaida wa dunia na kusababisha athari kwa mbinadamu na Maisha yao. 

Kuanzia kwenye sayari yetu hadi kwenye uchumi wa kimataifa. Janga hili la kibinadamu pia ni mfano wa jinsi gani nchi zisizojiweza , jamii na uchumi viko katika tishio kubwa.

Amezihimiza nchi kwamba “Ni lazima zifanye kila liwezalo kulinda afya ya wat una dunia ambavyo viko katika hatari kubwa sasa kuliko wakati mwingine wowote.”

Ameongeza kuwa mshikamano na hamasa vinahitajika sasa kuliko wakati mwingine wowote ili kuingia katika uchumi ambao una mnepo, endelevu, wenye hewa ukaa ndogo ambavyo vitadhibiti ongezeko la joto duniani kuhakikisha halizidi nyuzi joto 1.5C.

Katibu Mkuu ameahidi kuendelea kushirikiana bila kuchoka na waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson, nchi wanachama, asasi za kijamii, vijana na makampuni ya biashara ili kuhakikisha kwamba tunajikwamua vyema na kuibuka kidedea katika janga hili la kimataifa tukiwa imara.