Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF kuongeza msaada katika nchi 145 ili kuwezesha watoto kuendelea kujifunza, wakati huu wa COVID-19

Nchi zilizoendelea kama Marekani, watoto wanaendelea na masomo kwa njia ya mtandao wakiwa nyumbani katika kipindi hiki cha mlipuko wa virusi vya corona
© UNICEF/Lisa Adelson
Nchi zilizoendelea kama Marekani, watoto wanaendelea na masomo kwa njia ya mtandao wakiwa nyumbani katika kipindi hiki cha mlipuko wa virusi vya corona

UNICEF kuongeza msaada katika nchi 145 ili kuwezesha watoto kuendelea kujifunza, wakati huu wa COVID-19

Utamaduni na Elimu

Kufungwa kwa shule katika mataifa mbalimbali kukiingilia utaratibu wa masomo kwa zaidi ya asilimia 80 ya wanafunzi duniani kote, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF limetangaza hii leo kuwa litaongeza msaada wake kwa nchi zote ili kuwasaidia watoto kuendelea na ujifunzaji.

Mkuu wa kitengo cha elimu cha UNICEF duniani, Robert Jenkins amesema, “shule katika nchi nyingi zimefungwa. Ni hali isiyo ya kawaida na labda tuchukue hatua y pamoja ya kuilinda elimu ya watoto, vinginevyo jamii na uchumi vitakuwa na mzigo muda mrefu baada ya kuwa tumeitokomeza COVID-19. Katika jamii nyingi ambazo ziko hatarini, madhara yatabakia kwa vizazi.”

Aidha bwana Jenkins ametoa mifano kulingana na hali ambazo zimewahi kuikumba dunia akisema, “kwa kuzingatia mafunzo tuliyopata kutokana na kufungwa kwa shule wakati wa kupambana na Ebola, watoto wanavyokaa nje ya shule, ndivyo ambavyo pengine hawatarejea shuleni. Kuwapa watoto njia mbadala za kujifunza na kwa kufanya hivyo kunajenga mazoea ni jambo muhimu katika hatua zetu.”

Ili kusaidia kudhibiti usumbufu katika  elimu ya watoto na kuwafanya watoto wakiendelea kusoma kwa usalama, UNICEF imetenga nyongeza ya fedha ili kuendeleza kazi ya serikali nan a washirika katika zaidi ya nchi 145 za kipato cha chini na cha kati. Mgao wa kwanza wa dola milioni 13 za kimarekani, takribani dola milioni 9 zikiwa ni kutoka katika michango iliyotolewa na GPE ambao ni mfuko wa elimu, zitakuwa ni kichocheo kwa kusaidia serikali na wadau wa elimu katika kila nchi ili kuendeleza mipango kuwezesha hatua pana na za haraka katika mapambano ya kupata majibu ya mfumo mzima.

Mkakati huu utaziwezesha nchi kuandaa programu mbadala za ufundishaji wakati ambapo shule zimefungwa na hivyo kuwasaidia watoto waendelee kusoma na pia kuzifanya jamii zao zibakie salama kwa kuwapatia taarifa muhimu kuhusu kusafisha mikono na hatua nyingine za usafi. Fedha hizo zitasaidia pia katika afya ya akili ya watoto na pia kuzuia unyanyapaa na ubaguzi kwa kuhamasisha wanafunzi kuepuka mtazamo mbaya wanapoogelea virusi hivi vya corona.