Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

COVID-19 isiwe chanzo cha kusahau huduma muhimu za chanjo kwa watoto- UNICEF

Mama akiwa amembeba bintiye mchanga akimwandaa kwa ajili ya kupata chanjo kadhaa katika kituo cha chanjo kilichofadhiliwa na UNICEF katika jimbo la Kivu Kaskazini nchini DRC.
© UNICEF/Thomas Nybo
Mama akiwa amembeba bintiye mchanga akimwandaa kwa ajili ya kupata chanjo kadhaa katika kituo cha chanjo kilichofadhiliwa na UNICEF katika jimbo la Kivu Kaskazini nchini DRC.

COVID-19 isiwe chanzo cha kusahau huduma muhimu za chanjo kwa watoto- UNICEF

Afya

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limesihi serikali duniani kote kuanza mipango thabiti ya utoaji chanjo kwa watoto pindi janga la ugonjwa wa virusi vya Corona, au COVID-19 litakapodhibitiwa.
 

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF, Henrietta H. Fore ametoa kauli hiyo kupitia taarifa yake iliyotolewa leo mjini New York, Marekani, wakati huu ambapo amesema, “serikali zinaweza kuahirisha kwa muda kampeni za chanjo ili kuhakikisha kuwa kampeni hizo hazisababishi kuenea kwa virusi vya Corona kwa kuwa zinalazimika kuepusha mikusanyiko.”

Amesema kuwa duniani kote hivi sasa huduma za afya zimezidiwa uwezo na wahudumu wanaelekezwa katika kuhudumia wagonjwa wa COVID-19.

Halikadhalika amesema kuepusha mikusanyiko kunalazimisha zazi wafanya uamuzi mgumu kuhusu kufuatilia ratiba ya chanjo, huku vifaa vya matibabu navyo vikiwa ni haba, na mnyororo wa usambazaji wa bidhaa umevurugwa na kubadilishwa au kufutwa kwa ratiba za usafirishaji.

“Kufutwa kwa safari za ndege, vizuizi vya biashara navyo vimekwamisha upatikanaji wa dawa muhimu ikiwemo chanjo,” amenukuliwa Bi. Fore akiongeza kuwa, “kadri janga la virusi vya Corona linavyozidi kuenea, huduma muhimu za kuokoa maisha ikiwemo chanjo, zinaweza kuvurugika hususan katika nchi za Afrika, Asia na Mashariki ya Kati ambako ndiko zinahitajika zaidi.”

Ametanabaisha kuwa walio hatarini zaidi ni watoto kutoka familia maskini kwenye nchi ambazo taari zimeathiriwa na majanga ya asili na vita.

Mkurugenzi Mtendaji huyo wa UNICEF ametolea mfano ncih kama vile Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Ufilipino, Afghanistan, Somalia, Sudan Kusini na Syria ambako amesema “huku zikikabiliana na surua, kipindupindu au polio, sasa zinakabiliana tena na virusi vya Corona na hii si tu kwamba itadhoofisha mifumo afya bali pia inaweza kusababisha vifo na machungu.”

Amesema kuwa ujumbe ni dhahiri, “katu tusiruhusu hatua muhimu za kuokoa maisha zikaathiriwa na jitihada zetu za kutokomeza COVID-19.”

Ameongeza kuwa UNICEF kwa upande wake imejizatiti kusaidia mahitaji ya huduma muhimu za afya na chanjo katika nchi zilizoathirika zaidi na itafanya hivyo kwa njia ambamo kwayo haitasababisha kuenea kwa virusi vya Corona.