Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika ni wakati wa kuamka na kujiandaa na zahma ya COVID-19:WHO

Barabara ya UN jijini Nairobi nchini Kenya iko wazi wakati huu ambapo watu wanafanyia kazi nyumbani kuepuka kusambaza virusi vya corona.
UN Kenya/Newton Kanhema
Barabara ya UN jijini Nairobi nchini Kenya iko wazi wakati huu ambapo watu wanafanyia kazi nyumbani kuepuka kusambaza virusi vya corona.

Afrika ni wakati wa kuamka na kujiandaa na zahma ya COVID-19:WHO

Afya

Shirika la afya ulimwenguni WHO limetoa wito kwa bara la Afrika kuamka na kujiandaa na tishio kubwa la kimataifa za mlipuko wa virusi vya Corona , COVID-19. Katika mkutano wa kila siku na waandishi wa habari mjini Geneva mkurugenzi mkuu wa WHO Dkt. Tedros Adhamon Ghebreyesus amesema “kitu muhimu na bora kwa Afrika ni kujiandaa kwa zahma na kujiandaa sasa”

Akijibu swali la mwandishi wa habari kutoka Rwanda mkuu huyo wa WHO amesema hata kama kiwango cha wagonjwa wa virusi hivyo ni kidogo bado bara la Afrika linapaswa kujiandaa kwa janga kubwa. Ameongeza kuwa katika nchi nyingine tumeshuhudia jinsi gani virusi vikishika kasi baada ya kuzuka na kufikia kiwango cha juu, visa hivi vinayoelezwa ni idadi tunayotaka kuitumia kuhakikisha tunadhibiti ugonjwa huu kuanza shinani.

“Kwa sasa matukio ya COVID-19 kwa Afrika ni kidogo, lakini yanaweza kuongezeka kutokana na mapungufu ya upimaji, lakini Afrika bado ina fursa kubwa ya kuweza kuepuka athari kubwa za mlipuko huu na kuandaa umma wake na mifumo yake ya afya “ amesema Dkt.Michael Ryan mkurugenzi mtendaji anayehusika na udhibiti wa dharura za kiafya katika shirika la WHO.

Kwa kuzingatia hili wataalam wa WHO wanatarajia nchi za Afrika kusaka njia zozote zinazowezekana , kujifunza kutokana na uzoefu wan chi za asia na Ulaya ili kubaini njia ipi inawafaa.

Wakati huohuo shirika hilo la WHO limerejea ushauri wake wa umuhimu wa upimaji, kusaka watu waliokutana na waathirika, kuwatenda walioathirika na kuwatibu waliokumbwa na ugonjwa huo.

Kwa shirika hilo ni bayana kwamba wakati huu nchi zote ambazo zimekumbwa na COVIDI-19 ndani ya mia[aka yake lazima ziangalie hatua muafaka za kudhibiti watu kukutana hususani mikusanyiko mikubwa ambayo inauwezo za kusambaza ugonjwa huo.

 Afrika lazima iamke. Bara langu lazima liamke sasa-Dkt.Tedros.

Ili kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo WHOinaamini kwamba nchi zote ambako kuna maambukizi katika jamii zinatakuwa kufikiria kupunguza , kuchelewesha au kusitisha mikusanyiko mikubwa.

WHO imeonya kwamba mfano huo wa kuwaleta watu pamoja katika nwakati wa mlipuko kuna uwezekano wa kuusambaza zaidi ugonjwa hususani “katika mikusanyiko mikubwa ya kidini ambayo huwaleta watu pamoja kutoka sehemu mbalimbali.”

Mapendekezo ya WHO ni kuepuka kabisa mikusanyiko hii ya watu wengi na kuzuia virusi hivyo.

Dkt. Tedros amesisitiza kuwa “Kwa sababu tumeshuhudia jinsi gani COVID-19 inavyoweza kusambaa katika mabara mengine au nchi zingine hivyo Afrika iamke sasa. Bara langu linapaswa kuamka sasa.“ Ameongeza mkurugenzi huyo ambaye anatokea nchini Ethiopia barani Afrika.