Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

COVID-19 Tanzania: Wafanyabiashara ndogo ndogo wazungumza

Shughuli za ununuzi kwenye duka jijini Dar es Salaam, Tanzania wakati huu ambapo kumeripotiwa kutangazwa kwa visa vya corona nchini humo.
UN News/ Stella Vuzo
Shughuli za ununuzi kwenye duka jijini Dar es Salaam, Tanzania wakati huu ambapo kumeripotiwa kutangazwa kwa visa vya corona nchini humo.

COVID-19 Tanzania: Wafanyabiashara ndogo ndogo wazungumza

Afya

Nchini Tanzania  maambukizi ya virusi vya Corona au COVID-19 yameendelea ambapo hii leo wagonjwa wapya wawili wote wakazi wa Dar es salaam wamethibitishwa kuwa na virusi hivyo baaada ya mmoja kuingia nchini kutoka safari ya Denmark, Uswisi na Ufaransa huku mwingine akiwa amerejea kutoka Afrika Kusini.

Wagonjwa wote hao sasa wako chini ya uangalizi. Hayo yakiendelea baadhi ya wafanyabiashara ndogo ndogo wamezungumzia kile ambacho wanakumbana nacho huku wakisihi wananchi wazingatie hatua za kujikinga dhidi ya ugonjwa huo. 

Eneo la Mikocheni jijini Dar es salaam nchini Tanzania, wananchi wakiwa katika harakati za manunuzi wakati huu ambapo tayari taifa hili la Afrika Mashariki limethibitisha kuwa na wagonjwa wa virusi vya Corona.

Manunuzi yanafanyika huku baadhi wakiwa na barakoa kujikinga na Corona.

Katika viunga vya Namanga nako wilayani Kinondoni shughuli za zinaendelea za biashara na usafirishaji na kando tunakutana pia na mama lishe Binti Hassan ambaye yeye anazungumzia changamoto yao akisema kuwa, "sisi wafanya biashara wadogo wadogo tatizo letu ni moja, utoke ndio ujue kupate mkono kwenda kinywani,  Nawasihi wenzangu tuwemakini kwa vile wengine wanavaa   maglavu na barakoa. Hizi barakoa ata wakivaa wanazitoa kwa vile hawajazoe kwa hivyo wanatoa ili wapate hewa.Kwa hivyo naona kama hali ipo palepale."

Hata hivyo Binti Hassan amesema yeye akiwa ni mama lishe anahakikisha kuwa wateja wake wananawa mikono kwa sabuni ili kuepusha kusambaza virusi vya Corona na kwamba, "nasihi wafanyabiashara wenzangu wachukue hatua hiyo pia kuepusha ugonjwa huu."

Kwa mujibu wa shirika la afya ulimwenguni, WHO, hadi Jumatano kulikuwepo na wagonjwa 193, 475 waliothibitishwa katika nchi 164 duniani kote, na kati yao hao 7864 wamefariki dunia.