Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

COVID-19: Shule Tanzania zafungwa mikusanyiko isiyo ya lazima marufuku 

Kuosha mikono kwa sekunde 20 kunahamasishwa kama hatua za kukabiliana na virusi vya corona COVID-2019.
UN Photo/Loey Felipe
Kuosha mikono kwa sekunde 20 kunahamasishwa kama hatua za kukabiliana na virusi vya corona COVID-2019.

COVID-19: Shule Tanzania zafungwa mikusanyiko isiyo ya lazima marufuku 

Afya

Kufuatia kubainika kwa mgonjwa wa virusi vya Corona nchini Tanzania, taifa hilo la Afrika Mashariki limeanza kuchukua hatua kuepusha maambukizi zaidi ambapo hii leo limetangaza hatua kadhaa ikiwemo kufungwa kwa shule zote za awali, za msingi hadi sekondari kwa siku 30 kuanzia leo.  

Tangazo hilo limetolewa leo jijini Dar es salaam na Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa akisema, “Mikusanyiko yote mikubwa ya ndani na nje isiyo ya lazima imesitishwa kuanzia sasa ikiwemo shughuli za michezo, semina, matamasha ya muziki, mikutano mbalimbali ikiwemo ya shughuli za kisiasa, mahafali za shule na shughuli nyingine za kijamii ambazo si muhimu. Lakini pia tumefunga shule zote za awali, msingi na sekondari hadi kidato cha sita na zitafungwa kwa siku 30 kuanzia leo Machi 17, 2020.” 


Halikadhalika amesema kuwa, « na Wizara itafanya marekebisho ya ratiba ya kidato cha sita ambao wanatarajiwa kufanya mitihani tarehe 4 mwezi wa Mei. Watakuwa na muda mfupi kwa hiyo itasogezwa tena mbele kadiri ya matokeo yatakavyojitokeza ili nao wapate nafasi ya kusoma kwa kipindi kile kile kilichokubalika kwa mujibu wa ratiba hiyo. »

Mapema mara baada ya kutangazwa kuwepo kwa mgonjwa, shirika la afya ulimwenguni, WHO nchini Tanzania limepongeza hatua ya serikali ya kutangaza mapema uwepo wa mgonjwa likisema kuwani hatua ya kwanza ya kudhibiti kusambaa kwa mlipuko kwa mujibuwa kanuni za afya za kimataifa za mwaka 2005.

Mwakilishi wa WHO nchini humo Dkt. Tigest Ketsela Mengestu akizungumza na wanahabari amesema Tanzania ni nchi ya 25 barani Afrika kuwa na maambukizi na hivyo basi , “tunapenda kuwahakikishia usaidizi wa WHO na mfumo mzima wa Umoja wa Mataifa na jamii ya kimataifa. Kumekuwepo na uzoefu chanya China, Korea Kusini na Singapore. Tunaweza kudhibiti lakini tunahitaji kila mtu tushikamane katika hili. Tukishirikiana tunaweza kudhibiti.  Sasa ni mgonjwa aliyeingia na si kwamba umeanzia hapa ndani. Hatujaona maambukizi ya ndani . Hili ni muhimu sana kwa sababu kwa kufuatilia wale waliokuwa naye karibu tunaweza kudhibiti.”

Amesema kwa vyombo vya habari jukumu lao ni kusambaza habari za kweli na kwamba huu si wakati wa kuogofya, bali vyombo vya habari vitoe habar iza ukweli ili watu waweze kufahamu la kufanya ili kujikinga.